Friday, June 13, 2014

HII NDIYO NAMBA ILIYOTUMIKA KUMPIGIA MAREHEMU ERASTO MSUYA NA KUMUITA KWENYE TUKIO AMBALO LILIPELEKEA KUPIGWA RISASI: SOMA HAPA UIONE NAMBA HIYO

Bunduki ya kivita aina ya Sub Machine Gun (SMG) iliyotumika kumuua mfanyabiashara tajiri wa Mirerani, Erasto Msuya, ilinunuliwa kwa Sh4 milioni nchini Kenya, Mahakama imeelezwa.


Imeelezwa pia kwamba wauaji wanne waliokwenda eneo la tukio kutekeleza mauaji hayo, walilipwa Sh5 milioni kila mmoja na washirika wao wakilipwa Sh3 milioni kila mmoja.


Hayo yamo katika maelezo ya mashahidi 57 kwa washtakiwa yalisomwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa Kilimanjaro, Munga Sabuni juzi na mawakili wa Serikali, Stella Majaliwa na Florentina Sumari waliokuwa wakipokezana kuanzia saa 4:00 asubuhi hadi saa 11:00 jioni.


Msuya aliyekuwa anamiliki vitega uchumi kadhaa, aliuawa kwa kumiminiwa risasi Agosti 7, mwaka jana saa 6:30 mchana Mijohoroni wilayani Hai, Kilimanjaro na katika maelezo yake, mtaalamu aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu, Dk Paulo Christopher alisema ulikuwa na matundu 26 ya risasi yaliyotokana na risasi 13 zilizoingia na kutokea upande wa pili zikichanachana utumbo, mapafu, ubongo na bandama.


Ushahidi huo unadai kuwa katika eneo la tukio, polisi waliokota maganda 22 ya risasi za SMG.



Mtaalamu wa makosa ya kijinai ya kompyuta, Koplo William Obeid alieleza kuwa katika kufanikisha mauaji hayo, laini mpya tano za Airtel zilisajiliwa kienyeji, zote zikiwa na jina la Motiti Ndoole na laini iliyotumika kumvuta marehemu eneo la tukio ilikuwa 0682405323.


Katika ushahidi huo, Inspekta Samwel Maimu alidai kuwa washtakiwa walikiri kosa na kueleza kuwa bunduki aina ya SMG ilinunuliwa Namanga, upande wa Kenya. Inspekta Maimu alidai kuwa mshtakiwa wa kwanza, Shariff Mohamed ndiye aliyetoa Sh4 milioni za kununua silaha hiyo na kutoa fedha za kusajili line mpya tano za simu.


Pia alidai kuwa mshtakiwa huyo, ndiye aliyetoa Sh3,350,000 zilizotumika kununulia pikipiki mbili moja aina ya Toyo na nyingine King Lion zilizotumiwa na wauaji siku ya tukio.


Katika maelezo hayo yaliyosomwa mahakamani, mshtakiwa wa kwanza (Shariff), anadaiwa kueleza namna alivyotoa maagizo ya kusajiliwa kwa line mpya.


Mshtakiwa huyo anadaiwa kueleza kuwa mshtakiwa wa saba, Ally Mussa ndiye aliyemshauri atoe jiwe moja la Tanzanite litakalotumika kumshawishi marehemu Msuya. Katika maelezo hayo, ilidaiwa kuwa ndiye aliyelipa Sh4 milioni za kununua bunduki hiyo ya SMG na kwamba siku ya tukio aliibeba kwa gari lake hadi eneo la tukio na kuwakabidhi wauaji.
baadhi ya watuhumiwa wa mauaji hayo


Katika ushahidi huo, mshtakiwa wa tano, Karim Kihundwa anadaiwa kueleza kuwa yeye ndiye aliyemmiminia risasi marehemu ambazo hajui idadi yake na kwamba bunduki hiyo aina ya SMG waliinunua Namanga na ilihifadhiwa nyumbani kwa Shariff sambamba na pikipiki zilizotumika.




Katika maelezo yake, mshtakiwa wa saba, Ally Mussa au Majeshi anadaiwa kueleza kuwa ndiye aliyepewa kipande cha madini na kwenda kumuuzia marehemu hotelini kwake SG Resort siku moja kabla ya mauaji. 
Chanzo cha habari hii ni Libeneke la Kaskazini

No comments:

Post a Comment