
“Ukistaajabu
 ya Musa utayaona na Firauni” ni maneno ambayo yamekuwa yakitumiwa na 
watu mbalimbali hapa nchini, yenye lengo la kuikumbusha jamii fulani juu
 ya yale yanayotokea kwa wakati huo.
Maneno
 haya, nimelazimika kuyakumbuka katika makala haya kutokana na tukio 
lililotokea wilayani Geita wiki iliyopita, ambapo gari la kubeba 
wagonjwa lilikamatwa likiwa linatumika kubeba mafuta ya wizi katika 
mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).
Kamanda
 wa Polisi Mkoani Geita, Leonard Paulo, anazungumzia tukio hilo kuwa 
lilitokea Septemba 5, mwaka huu saa saba usiku likiwa na lita 630 za 
mafuta zenye thamani ya sh.mil 1.3.
Analitaja
 kuwa ni lenye namba za usajili T.671 AKW aina ya Land Cruiser ambalo ni
 la kituo cha afya cha Nzera katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
Anasema
 lilikuwa likiendeshwa na Bw.Amud Bihemo (28) ambapo lilikuwa 
limefunikwa maandishi yanayotoa utambulisho wake kuwa ni gari la 
wagonjwa kituo cha afya Nzera na mengineyo kama vile alama ya msalaba 
mwekundu ili lisitambulike kwa urahisi.
“Limekamatwa
 na polisi kwa kushirikiana na walinzi wa mgodi huo, likiwa mgodini 
katika eneo la kufua umeme wa mgodi lijulikanalo kama Geita power, huku 
maandishi yanayolitambulisha kama gari la wagonjwa Nzera yakiwa 
yamefunikwa kwa karatasi za mng’ao na ile sehemu ya kubebea mizigo nayo 
ikiwa imeng’olewa pamoja na kimulimuli chake ambapo pia waliweka 
kitambaa cha kuakisi mwanga ili lifanane na yale ya mgodi huo,” anasema 
Kamanda Paulo.
Anawataja
 watuhumiwa wengine ambao walikamatwa eneo la tukio kuwa ni Bw.Malemo 
Paul (38), Bw.Seleman Magoso (31), Bw.Julias Boas (28), Bw.Rashid 
Hussein (27) na Ismail Zuberi(26) wote walinzi wa kampuni ya ulinzi ya 
G4S.
Wengine
 ni Bw.Christopher Kombo(26), mfanyakazi wa mgodi huo na Joseph 
Christopher na kwamba watuhumiwa wengine walifanikiwa kutoroka.
Kwa
 hakika tukio hili, linawagusa watu wengi si wilayani humo pekee bali 
hata katika mikoa mingine hasa kwa wananchi waishio maeneo ya vijijini, 
ambao wamekuwa wakitaabika kutokana na huduma duni za usafiri pindi 
wanapokabiliwa na matatizo ya kiafya.
Gari
 hili la kubeba wagonjwa ni msaada uliotolewa na mgodi wa dhahabu wa 
Geita (GGM) mwezi Desemba mwaka jana, likiwa na thamani ya sh.mil. 40 
ili kusaidia kuondoa kero ya wananchi wanaopata huduma ya matibabu 
katika kituo cha afya cha Nzera.
Kituo
 hiki cha afya ambacho kiko umbali wa zaidi ya kilomita 40 kufika ulipo 
mgodi huu, kinategemewa na idadi kubwa ya wananchi wanaoishi katika 
tarafa ya Bugando yenye kata sita ambazo ni Nzera, Senga, Nkome, 
Muharamba, Fulwe pamoja na Ruenzela.
Kwa
 mjibu wa sera ya afya, kituo hiki kimelenga kutoa huduma kwa wananchi 
wapatao 34,812 ambao ni kutoka kata ya Nzera pekee na ndio walistahili 
kuhudumiwa na gari hili lakini kutokana na upungufu wa magari ya 
wagonjwa limekuwa likitoa huduma na maeneo mengine ndani ya tarafa hii.
Baadhi
 ya familia zinazoishi katika maisha duni, zimekuwa zikilazimika kutumia
 usafiri wa baiskeli na nyingine kutumia mikokoteni inayokokotwa kwa 
punda ili kuwawezesha wagonjwa wao kuzifikia huduma za afya kama vile 
zahanati, vituo vya afya ama hospitali za wilaya na zile za rufaa.
  Usafiri
 wa aina hii mara nyingi umekuwa ukisababisha vifo vya mara kwa mara 
hasa kwa akina mama wajawazito wanapopatwa matatizo wakati wa kujifungua
 pamoja na watoto ambao wamekuwa wakisumbuliwa na tatizo kubwa la 
ugonjwa wa malaria.
   Tukio
 hili la gari la wagonjwa kutumika katika shughuli za wizi kinyume na 
matarajio ya serikali na wananchi kwa ujumla, maoni tofauti yametolewa 
huku mambo mapya yakijitokeza.
  Wananchi
 wa Nzera ndio hasa walioguswa na tukio hili kwa kile wanachokiona kuwa 
hali ya afya zao iko shakani kutokana na hujuma kama hizi za matumizi 
yasiyo sahihi ya magari ya kubeba wagonjwa.
“Taarifa
 hizi binafsi zilinihuzunisha mno, tumekuwa katika mateso makubwa kabla 
ya kuletwa katika kituo hiki, lilikuwa msaada kwetu kwani kuna familia 
nyingine hazina fedha kwa ajili ya kukodi gari kutoka hapa Nzera hadi 
hospitali ya wilaya ya Geita, hivyo lilikuwa linatusaidia kwa kweli hasa
 sisi kina mama,” anaeleza kwa masikitiko Bi. Verediana Nestory mkazi wa
 Nzera katika mazungumzo na mwandishi wa makala haya aliyetembelea 
kijijini hapo.
  “Tunapata
 shida lisipokuwepo hili gari la wagonjwa, watu wengi watapoteza maisha 
kwa sababu tu ya kushindwa kupata huduma mapema kutokana na kutokuwa na 
fedha, mfano huko nyuma kabla halijaletwa hapa kuna jirani yangu 
niliwahi kumshuhudia akiweka dhamana ya mbuzi ili apate gari ya kukodi 
toka kwa mtu binafsi ili mgonjwa wake apelekwe hospitali ya Wilaya ya 
Geita,” anaongeza.
  Anasema,
 jirani yake huyo aliyeweka dhamana ya mbuzi hakuwa na fedha kwa ajili 
ya kulipa usafiri wa gari ili kumuokoa binti yake aliyekuwa na tatizo la
 kujifungua, ambapo mumewe alimtelekeza na kukimbilia kusikojulikana.
  Mwanamke
 mwingine ambaye hakutaka kutaja jina lake gazetini, mfanyabiashara ya 
duka jirani na ulipo mgahawa aliokuwa akipendelea dereva wa gari hilo la
 wagonjwa kijijini hapo, anasema wao wanachotaka gari hilo lirejeshwe 
katika kituo hicho cha afya.
 “Kama
 ni wizi amefanya dereva kwa tamaa zake sawa lakini tunachotaka sisi 
wananchi wa Nzera, gari letu la wagonjwa waturudishie tu, kwani lilikuwa
 likisaidia watu wengi katika maeneo haya ya tarafa nzima ya Bugando, 
haiwezekani kosa afanye dereva halafu wananchi tuadhibiwe kwa kukosa 
huduma,” anasema.
  Baadhi
 ya wananchi walisema kuwa licha ya kuwa gari hilo lilitakiwa kutoa 
huduma hiyo bure, lakini baadhi yao walikuwa wakitozwa fedha kati ya 
sh.10,000 hadi 30,000 kama gharama ya kuchangia mafuta, fedha ambazo 
zinasadikika zilikuwa zikichukuliwa na dereva wa gari hilo.
  Kwa
 mujibu wa Mganga Mfawidhi wa kituo hicho cha afya Nzera, Dkt. Bahati 
Nyamachaguri ni kuwa kabla ya tukio hilo la kukamatwa kwa gari hilo la 
wagonjwa, kuna mgonjwa aliyemtaja kwa jina la Domicia Kabale (56) 
alikuwa amelazwa kituoni hapo na alipatwa na tatizo la kupooza mdomo 
ambapo alilazimika kupelekwa hospitali ya wilaya ya Geita kwa matibabu 
na uchunguzi zaidi.
  “Tulilazimika
 kulitumia gari hili la wagonjwa mimi ndiye niliongoza msafara na ndani 
ya gari tulikuwemo watu wanne akiwemo mgonjwa na ndugu yake, kwa kuwa 
kesho yake nilitakiwa kuchukua dawa za kupunguza ugonjwa wa virusi vya 
Ukimwi(VVU).”
  “Tulifika
 salama saa 11 hivi jioni ya siku hiyo, mgonjwa akapokelewa na wenzetu 
wa hospitali ya wilaya na kwa mujibu wa sheria niliamini gari hilo 
litabaki hapo hospitali hadi kesho yake,” anaongeza.
  Anasema,
 kesho yake asubuhi wakati anafika hospitalini hapo akijiandaa kwenda 
kuchukua dawa hizo lili arudi kituoni kwake kwa kulitumia gari hilo, 
alishangaa baadhi ya madereva waliokuwa wamekusanyika wote wakiwa 
wameelekeza macho yao kwake na baadaye aliambiwa kuwa gari la kituo 
chake cha Nzera liko kituo cha polisi baada ya kukamatwa likifanya 
uhalifu mgodini.
  “Nilienda
 kituoni pamoja na mkurugenzi, tulikuta kweli gari liko hapo polisi, 
likiwa limezibwa maandishi kwa stika, sehemu ya juu ya kubebea mizigo 
imeng’olewa na imewekwa kitambaa cha mng’ao kama yale ya mgodini, 
nilibaki kushangaa.” anasema.
  Mganga
 huyo Mfawidhi, anasema gari hilo huwa linawekewa mafuta kila siku ya 
Jumatatu kutoka ofisi ya Halmashauri ya wilaya na kuwa tukio hilo 
alilosema kuwa siyo zuri limemuumiza yeye binafsi.
 “Kwa
 kweli limenipatia fundisho kubwa wananchi walikuwa wamelizoea kutokana 
na kuwa msaada wao mkubwa ingawa wapo baadhi ya viongozi wa kisiasa 
walikuwa wakitoa vitisho kwa dereva pindi anapogoma kufanya yale 
wanayotaka ikiwemo kubeba wagonjwa wao pasipo kupitia ngazi zinazohusika
 za uongozi. Hii inatokana na baadhi ya watu kutojua utaratibu.
  Mwandishi
 wa makala haya akiwa kituoni hapo, alishuhudia mume na mke waliokuwa na
 mtoto wao aliyekuwa na tatizo la kuishiwa damu kwa mjibu wa daktari, 
wakibaki kuangua kilio kutokana na kushindwa gharama ya nauli ya 
sh.4,000 ili kumfikisha mtoto huyo hospitali ya wilaya ya Geita kwa 
matibabu.
  Majira
 iliweza kubaini kuwa katika kituo hicho, hapakuwepo na kitabu cha 
makabidhiano kwa ajili ya kusaini pindi gari hilo linapoingia ama kutoka
 ambapo dereva wake pia hakuwa mtumishi wa kudumu wa Halmashauri hiyo 
bali alikuwa akifanya kazi kama kibarua (cassual) aliyekuwa akisaini 
mkataba kila baada ya miezi mitatu.
  Mmoja
 wa dereva basi dogo la abiria maarufu kama Hiace linalofanya safari 
zake kutoka mjini Geita kwenda Nkome kupitia kijijini hapo, ambaye 
hakutaka kutaja jina lake kwa usalama wake, anasema mara nyingi gari 
hilo la wagonjwa amekuwa akilikuta limeegeshwa porini jirani na eneo la 
mgodi wakati wa usiku.
  “Hawa
 bwana watakuwa wamedhulumiana wao kwa wao tu ni mara nyingi pengine 
limekuwa likitumika kwa shughuli kama hizi hasa usiku, nimekuwa 
nikikutana nalo limeegeshwa hapa porini usiku, siku zimefika mwisho, 
dogo amechezea kazi ningelikuwa na ndugu yangu huko wizarani 
ningelimpigia nipate hiyo nafasi,” anasema.
  Naye
 mlinzi mmoja wa kampuni ya Intensive Security inayotoa huduma ya ulinzi
 katika hospitali ya wilaya ya Geita(jina limehifadhiwa), anasema siku 
ya tukio dereva huyo aliwaeleza kuwa yuko zamu ya usiku, hivyo gari lake
 litakuwa na mizunguko ya mara kwa mara kutoka nje na kuingia lango kuu 
la hospitali hiyo ya wilaya.
  “Unajua
 bwana yaani unaweza kudanganya sana lakini kama siku imefika imefika 
tu, siku hiyo alikuja hapa getini na kutueleza yuko zamu na kama kawaida
 tuna vitabu huwa tunaweka kumbukumbu yaani siku hiyo alianza kutoka saa
 2 usiku na kuingia mara nyingi kweli hadi tukachoka kufungua geti 
tukalazimika kuliacha wazi na mara ya mwisho alitoka saa 7 
usiku,”anasema mlinzi huyo wa Kampuni ya Intensive Security na kuwa 
kuruhusiwa kwa gari hilo kunatokana na magari ya wagonjwa wakati 
mwingine kutumika kuwapeleka madaktari nyumbani kwao pindi wanapomaliza 
kazi za kuhudumia wagonjwa.
Mkuu wa Mkoa na wilaya nao wanena
    Mkuu
 wa Mkoa wa Geita, Bw. Magalula Said Magalula, katika mazungumzo na 
waandishi habari ofisini kwake, amewataka madereva na viongozi wa 
serikali kuacha kutumia vibaya mali ya umma kwa kuwa ni aibu.
   Mkuu
 wa Wilaya ya Geita, Bw. Manzie Omary Mangochie, anasema tukio hilo 
limemshtua mno na kwamba hakuwa na mawazo kuwa kuna siku ataliona gari 
la wagonjwa likiwa linatumiwa katika vitendo vya wizi badala ya kufanya 
kazi yake ya kubeba wagonjwa.
  “Nimesikitika
 sana, binafsi nimelazimika kufika kituoni mwenyewe kuona kitendo hiki 
cha fedheha! Lazima hatua zichukuliwe kamwe hatutokubali vitendo vya 
namna hii viendelee katika wilaya yetu, nimeagiza hatua kali zichukuliwe
 mara moja,”anasema mkuu huyo wa wilaya kwa masikitiko makubwa.
Kauli ya uongozi wa Halmashauri
  Kwa
 upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Bw. Ali 
Kidwaka, anakiri kuwa ni kweli dereva huyo alikuwa kibarua kwa muda wa 
mwaka mmoja sasa.
“Niliunda
 timu maalumu kufuatilia mara baada ya tukio hili na ilifahamika dereva 
hakuwa mwajiriwa wa kudumu wa Halmashauri, lakini pia limetupatia 
fundisho na angalizo kubwa,” anasema.
 “Gari
 la wagonjwa kutumika katika wizi kama huu bila shaka hata wewe 
mwandishi hili wazo sidhani kama ulikuwa nalo kuwa inaweza kuwa, ndivyo 
hivyo hata mimi lakini kuanzia sasa tunaanza kufanya ufuatiliaji magari 
yote ya serikali katika Halmashauri, tutatoa waraka kama njia ya 
kudhibiti na kweli tutafanya hata ziara za kushtukiza,” anaongeza.
  Anasema,
 kwa sasa Halmashauri hiyo yenye vituo vya afya vitano ambavyo ni 
Katoro, Chikobe, Kashishi, Bukoli na Nzera inakabiliwa na upungufu 
mkubwa wa magari ya kubeba wagonjwa ambayo yaliyopo sasa ni mawili 
pekee.
  Kwa
 mjibu wa taarifa ya maombi maalumu yaliyopelekwa Wizara ya Fedha kwa 
Halmashauri hiyo mwaka 2011, jumla ya sh.mil. 420 zilikuwa zimeombwa kwa
 lengo la kununua magari matatu ya kubeba wagonjwa, maombi ambayo 
hayakukubaliwa.
  Maombi
 hayo yalikuwa yamelenga kurahisisha utoaji wa huduma kwa haraka ikiwa 
ni pamoja na kuokoa maisha ya wananchi wilayani humo.
Mwenyekiti
 wa Halmashauri hiyo, Bw.Elisha Lupuga anasema “dereva huyu lazima 
afukuzwe kazi mara moja na kutokana na tukio hili jana tumefanya kikao 
na madereva wote wa Halmashauri, tumeonya kuwa endapo litajirudia 
hatutawafumbia macho wale wote watakaopatikana wakijihusisha na vitendo 
hivi,” anasema.
  “Suala
 la kwamba dereva alikuwa mwajiriwa wa muda si hoja bali hata kama 
angelikuwa ameajiriwa angefanya hivyo kama ni tabia yake, hivyo lazima 
hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria,” anaongeza mwenyekiti huyo.
Viongozi wa vyama vya siasa wanazungumziaje tukio hili?
  Katibu
 wa Itikadi, Siasa na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) mkoani Geita, 
Bw.Said Kalidushi anasema kuwa tukio hilo ni sawa na hujuma kwa wagonjwa
 ambao ndio wanaolitegemea zaidi.
  “Ni
 hujuma kwa wagonjwa, mfano endapo pangelikuwepo na mgonjwa ambaye 
alitakiwa kutolewa kituoni hapo kwenda hospitali ya wilaya ya Geita kwa 
matibabu zaidi ina maana angelipoteza maisha kutokana na hujuma kama 
hizi.”
  “Siamini
 inakuwaje gari la wagonjwa liende mgodini kuiba mafuta badala ya 
kuhudumia wagonjwa? CCM imekuwa ikilalamikiwa kwa matukio kama haya, 
hizi ni tamaa zake na gari hili lilitolewa na mgodi na hilo hilo ndilo 
limeenda kuiba humo ndani yaani hii ni sawa na mbwa anayemng’ata mfugaji
 wake...” anasema na kuongeza kitendo hicho kisiwavunje wafadhili bali 
waendelee kutoa misaada kwa jamii pale wanapoona inafaa kuwa hivyo.
Msemaji
 wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) mkoani Geita, Ignas 
Karashani, anasema kuwa serikali inatakiwa kufanya uchunguzi wa kina ili
 kubaini endapo kitendo cha gari hilo kwenda kufanya wizi mgodini 
kilikuwa na shinikizo toka kwa kiongozi yoyote ili hatua zichukuliwe 
mara moja.
  “Kazi
 ya gari hili ni kubeba wagonjwa kwa dharura, huko nani aliamuru liende?
 Pale Nzera kuna diwani ambaye ni Musukuma kama diwani naye alipaswa 
kufuatilia kwa karibu kwa sababu linahudumia watu wake, lazima naye 
ahojiwe huenda alishinikiza kwa maslahi yake,” anasema Diwani wa kata ya
 Nzera ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM mkoani humo, Bw.Joseph Musukuma 
yeye alitupia lawama Mganga Mfawidhi wa kituo hicho pamoja na dereva 
kuwa wanastahili kuwajibika.
  “Mganga
 Mkuu na dereva wote wanatakiwa kwenda jela tu hao,” alimaliza kisha 
kukata siku kwa kile alichoeleza alikuwa akiendelea na mkutano.
Uongozi wa mgodi
  Kaimu
 Mkurugenzi Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), Bw. Jasper Musadaidzwa, 
katika taarifa yake kwa vyombo vya habari anasema kuwa mgodi huo 
umeshtushwa na tukio hilo la wizi uliofanywa kwa kutumia gari la kubeba 
wagonjwa.
  Anasema,
 mgodi huo ulitoa msaada wa gari hilo, kwa lengo la kusaidia kusafirisha
 wagonjwa, watoto na akina mama wajawazito kwa kuzingatia moja ya sera 
ya afya ya mgodi huo isemayo wananchi lazima wanufaike na uwepo wao.
  “Tumeshtushwa
 na wizi huu ambao umefanywa na watu wachache ambao wanatumia rasilimali
 za umma kwa matumizi yao binafsi badala ya kuokoa maisha ya watu,” 
anasema mkurugenzi huyo wa GGM.
  Kukamatwa
 kwa gari hilo la wagonjwa likiiba mafuta mgodini humo, kumeleta hofu 
kubwa kuwa huenda pengine yapo baadhi yanatumika katika usafirishaji 
dawa za kulevya kwa kuwa si rahisi kukaguliwa na polisi kwa kudhaniwa 
yamebeba wagonjwa.
  Takwimu
 zinaonesha kuwa Tanzania inakabiliwa na uhaba mkubwa wa magari ya 
kubeba wagonjwa katika vituo na hospitali mbalimbali, hali ambayo 
ilisababisha Rais Jakaya Kikwete wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 
2010, kuahidi kusambaza pikipiki za matairi matatu (bajaji) zipatazo 
400,000 nchini.
  Katika
 ahadi hiyo, Rais Kikwete alisema lengo ni kusaidia wagonjwa hususani 
wanawake wajawazito kuwahishwa hospitali wakati wa kujifungua.
  Kwa
 mujibu wa sera ya afya ya mwaka 2007, Serikali kwa kushirikiana na 
wadau mbalimbali itahakikisha utoaji wa huduma bora za uzazi katika 
vituo vya kutolea huduma za afya zinazowavutia wanawake, wanaume na 
vijana hapa nchini
Majira
No comments:
Post a Comment