Friday, September 14, 2012

MBOWE WA NECTA ASIMAMISHWA KAZI

Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imemsimamisha kazi na itamchukulia hatua za kinidhamu Mkuu wa Idara ya Utafiti, Tathmini na Huduma za Kompyuta, Joseph Mbowe baada ya uchunguzi kubaini kuwapo kwa dosari katika ukokotoaji wa alama za mitihani ya somo la Islamic Knowledge katika kompyuta.

Aidha, Wizara hiyo imeagiza NECTA kukokotoa upya alama za mitihani ya wanafunzi wa kidato cha sita ya somo hilo waliofelishwa kwa bahati mbaya mwaka huu kutokana na dosari hiyo na tayari matokeo ya alama hizo yametolewa.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo na Ufundi, Philip Mulugo alisema Mei 28, mwaka huu, Wizara ilipokea malalamiko kutoka Baraza la Wakuu wa Shule za Kiislamu, dhidi ya matokeo ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka huu katika somo hilo.

Alisema baada ya Serikali kupokea malalamiko hayo iliunda tume ya watu tisa ikijumuisha wajumbe kutoka Wizara ya Elimu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Wizara ya Elimu na Amali Zanzibar, Necta, Baraza la Elimu la Kiislamu, Baraza la Wakuu wa Shule za Kiislamu, Idara ya Usalama wa Taifa na Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Alisema kamati hiyo ilitakiwa kupitia orodha ya wasahihishaji wa somo hilo, kupitia maoni ya wasahihishaji, sampuli za mitihani za watahiniwa, kuhakiki uhamishaji wa alama kutoka mitihani kwenda kwenye kompyuta na kulinganisha mchakato wa usahihishaji na matokeo ya somo hilo kwa mwaka huu na miaka ya nyuma.

Mulugo alibainisha kuwa baada ya uchunguzi wa kamati hiyo ilibaini kuwa ukokotoaji wa alama za mitihani ya somo hilo ulikuwa na dosari kutokana na mfumo uliotumika kukokotolea kutofanyiwa marekebisho kulingana na mabadiliko ya sasa.

“Miaka ya nyuma somo hili lilikuwa linafanywa mitihani mitatu ambapo mfumo wa kompyuta ulikuwa unakokotoa na kugawanya alama kwa kutumia idadi hiyo ya mitihani mitatu, lakini mwaka huu tumebadilisha na mitihani ya somo hili ni miwili, lakini ukokotoaji uliotumika ni wa zamani wa kugawanya kwa mitihani mitatu,” alisema.

Alisema baada ya matokeo hayo, Serikali imeagiza Necta imchukulie hatua za kinidhamu Mbowe ambapo pia tayari wanafunzi waliofelishwa kutokana na dosari hiyo, alama zao za mitihani zimekokotolewa upya kwa mfumo wa sasa.

Sakata la kufeli kwa wanafunzi wa somo hilo mwaka huu, liliibua mjadala mkubwa ambapo Jumuiya na taasisi za Kiislamu zilifikia hatua ya kutaka Mkurugenzi Mtendaji wa Necta, Dk Ndalichako na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa wajiuzulu kutokana na uzembe uliotokea.