Friday, September 14, 2012

WANANCHI WATAKA KATIBA MPYA IRUHUSU WANANCHI KUVUTA BANGI

KATIKA hali ya kustaajabisha wananchi na hata wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, mkazi wa Kijiji cha Kingerikiti, Kata ya Kingerikiti, wilayani hapa, Jackson Mbunda (35), ameitaka Katiba mpya iruhusu uvutaji bangi nchini.

Amesema, maoni yake hayo yanazingatia ukweli kwamba, bangi ni aina mojawapo ya tumbaku na kiburudisho na anashangaa kwa nini sigara imeruhusiwa lakini bangi imepigwa marufuku.

Akitoa maoni yake jana, katika Kata ya Kingerikiti mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mbunda alisema, “Napendekeza kuwa bangi iruhusiwe kwa vijana lakini iwekewe maelezo kama yalio kwenye sigara.”

Mbunda akisimamia maoni yake hayo yaliyosababisha miguno kwa wananchi waliohudhuria mkutano huo na hata baadhi ya wajumbe wa Tume, alisema sababu ya kupendekeza hayo ni kutokana na hali halisi kuwa vijana wanazidi kuharibika kwa kuwa wanavutia uchochoroni.

“Nashangaa kwa nini sigara inaruhusiwa lakini bangi inapigwa vita, sijui kama serikali inafahamu kuwa vijana wengi wanavuta bangi kwa makosa huko vijiweni na uchochoroni, hawa wangewekewa maelekezo ya namna ya kuvuta bangi na ikawa ruksa, wasingeharibika kama ilivyo sasa,” alisisitiza Mbunda.

Alisema mpaka sasa takwimu za vijana wanaoharibika kwa bangi na dawa nyingine za kulevya ni wengi lakini ikiwa itaruhusiwa kisheria na kuwapa vijana maelekezo ya namna ya kutumia, wataweza kufanya kazi na kuingiza kipato badala ya muda mwingi kuutumia kwenye vificho.

Hata hivyo, Wajumbe wa Tume hawakumuuliza ufafanuzi wowote kama ilivyo kawaida.

Awali, Mwenyekiti wa msafara ulioko mkoani Ruvuma, Profesa Mwesiga Baregu aliwataka watoe maoni bila wasiwasi wowote.