Tuesday, July 10, 2012

CHADEMA WAMJIBU NCHIMBI

Dk Slaa pia alitoa tamko  ambalo limepitishwa na Kikao cha Kamati Kuu iliyokutana tangu juzi kuhusiana na mpango wa usalama wa Taifa kutaka kuwadhuru viongozi wa CHADEMA, Dk. Slaa amesema hawaoni sababu ya kuhojiwa na Jeshi la Polisi kwa kuwa wamewahi kuwapa taarifa nyingi za vitisho dhidi yao na hakuna hata moja imefanyiwa kazi.

“Hatuwezi kwenda Polisi kwa sababu tumekuwa tukipeleka mambo mengi ya vitisho lakini hayafanyiwi kazi…na hili tulisha waambia hatuendi kwao labda watukamate,” alisema Dk. Slaa akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema yeye mwenyewe licha ya kuwasilisha madai mbalimbali aliwahi kutegeshewa vinasa sauti na kutoa taarifa polisi lakini tangu wachukue vifaa hivyo hawajasema chochote hadi leo, jambo ambalo limewafanya waamini hata wakienda huko hakuna chochote kitafanyika.

Dk. Slaa alisema leo asubuhi alipigiwa simu na mmoja wa maofisa upelelezi kutoka Makao Makuu ya Polisi akiomba miadi ya kukutana naye, jambo ambalo amesema hayupo tayari kuhojiwa na wanausalama hao wa raia labda wamkamate.

Alisema tayari baadhi ya viongozi wa Serikali wameanza kuipuuza malalamiko yao dhidi ya vitisho wakidai huenda viongozi wa CHADEMA wanatafuta umaarufu wa kisiasa kwa kutoa taarifa hizo, kitendo ambacho amesema umaarufu wao hautatokana na viongozi wa Serikali au CCM bali ni kwa kazi wanazozifanya kwa wananchi.

Juzi Dk. Nchimbi alisema taarifa za kutishiwa maisha dhidi ya viongozi wa CHADEMA ni nzito hivyo haziwezi kupokelewa kirahisi Jeshi la Polisi linaanza kazi ya kuwahoji wahusika ili kulifanyia kazi jambo hilo. Alisema suala la usalama wa raia si hiyari bali ni la lazima hivyo hata kama wahusika hawataki lazima taratibu zifanywe kuhakikisha usalama kwa wahusika.

Baadhi ya waandishi wa habari waliohudhuria kwenye mkutano huo.