Friday, April 13, 2012

WANAWAKE WA TWIGA STARS WATACHEZA NA WANAUME WA BONGO MUVI J2



 Kikosi cha Bongo Movies
Kikosi cha Twiga Stars

Timu ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Twiga Stars) itacheza mechi ya kirafiki na timu ya wasanii wa filamu ya Bongo Movie itakayofanyika Jumamosi (Aprili 14 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
Lengo la mechi hiyo ya maonesho (exhibition) ni kuichangia Twiga Stars ambayo hivi sasa iko kwenye mashindano ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) ambayo fainali zake zitafanyika Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea. 
Pia asilimia mbili ya mapato yatakayopatikana kwenye mechi ya Twiga Stars na Bongo Movie yatakwenda kwenye familia ya mwigizaji nguli wa filamu Tanzania, Stephen Kanumba aliyefariki dunia Aprili 7 mwaka huu. 
Kiingilio katika mechi hiyo kitakuwa sh. 10,000 kwa VIP A, sh. 5,000 kwa VIP C na B na sh. 2,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, kijani na bluu. Mechi itaanza saa 10 kamili jioni. 
Twiga Stars itacheza mechi ya kwanza ya mchujo dhidi ya Ethiopia jijini Addis Ababa. Mechi hiyo itachezwa Mei 26 mwaka huu na wiki mbili baadaye timu hizo zitarudiana jijini Dar es Salaam. Twiga Stars ilifuzu raundi hiyo baada ya kuitoa Namibia kwa jumla ya mabao 7-2.