Saturday, April 13, 2013

SERIKALI KUENDELEA KUWAAJIRI WASTAAFU

Akijibu swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Musoma Mjini, Vicent Nyerere (CHADEMA) aliyehoji Serikali ina mpango gani wa kusitisha kutoa Mikataba kwa wastaafu ili wahitimu wanaotoka vyuoni wapate ajira, waijenge nchi yao Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani amesema Serikali itaendelea na utaratibu wa kuwaajiri wastaafu katika kada za uhandisi, ualimu, uganga na wahadhiri wa vyuo vikuu mpaka hapo soko la ajira litakapojitosheleza.

“Hilo linatokana na utaalamu walionao ambao ni vigumu kuziba nafasi zao kwa kipindi cha haraka.” alisema Kombani.

Waziri alisema ni kweli kuwa wako wataalamu wengi wanaohitimu vyuo vikuu hapa nchini ambao wanahitaji kuingia katika soko la ajira, lakini hupatiwa ajira kulingana na uwezo na bajeti ya Serikali.

Kwa sasa Serikali inawapa mikataba ya muda mfupi wataalamu wastaafu wa kada hizo ambao sio rahisi kuwapata katika soko la ajira, sanjari na kuwaajiri wahitimu wa vyuo mbalimbali. Waraka wa Rais namba 1 wa mwaka 1998 unatamka kwamba endapo utaalamu wa mtumishi unahitajika sana, Serikali inawajibika kumwomba mtumishi kuendelea kufanya kazi na siyo mstaafu mwenyewe kuomba.

Katika swali la nyongeza la Nyerere kuwa Wakuu wa mikoa wengi ni wastaafu lakini wameajiriwa serikalini, Kombani alisema, “wakuu wa mikoa si watumishi wa umma na wapo katika utumishi wa kisiasa kama walivyo wabunge”.

Katika swali la nyongeza, Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR Mageuzi) aliyetaka kufahamu kwa nini Serikali haijawaajiri walimu waliomaliza Shahada ya Ualimu katika Saikolojia katika Chuo cha Ualimu Dar es Salaam (DUCE) wakati ilipoajiri walimu wengine, Kombani alijibu, “Kweli mwanzoni tulipoajiri wao hatukuwaajiri lakini sasa Serikali inafanya utaratibu ili iwapangie kazi wahitimu hao”

 

No comments:

Post a Comment