Tuesday, October 9, 2012

MWINYI APANDA KIZIMBANI KUTOA USHAHIDI WA KUIBIWA MILIONI 37

Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi jana alipanda kizimbani katika kesi ya wizi wa kuaminika wa Sh milioni 37.4 inayomkabili Abdallah Mzombe (39), ambaye alikuwa mfanyakazi wake huku wanahabari wakizuiwa kusikiliza.

Mzombe alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam Agosti 21 akidaiwa kuwa katika siku tofauti kati ya Januari mosi na Julai 10, akiwa wakala wa kukusanya kodi kwenye nyumba za Mzee Mwinyi, aliiba Sh milioni 17.6.

Inadaiwa aliiba fedha hizo za kodi ya mwaka 2011/12 na 2012/13 alizokuwa amekusanya kutoka kwa mpangaji wa nyumba namba 481 ya Mikocheni.

Katika mashitaka mengine, Mzombe anadaiwa kuiba Sh milioni 19.8 za malipo ya kodi ya mwaka 2011/12 na 2012/13 ya mpangaji wa nyumba namba 55 ya Msasani Village.

Hakimu Gane Dudu aliahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 22 kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa na mshitakiwa alirudishwa rumande.

Katika hali isiyo ya kawaida, walinzi wa Mzee Mwinyi walizuia waandishi wa habari kuingia mahakamani kusikiliza ushahidi aliokuwa akiutoa na Rais huyo mstaafu.

Mwinyi alifika mahakamani hapo na kuingia kwenye chumba cha Mahakama saa 5 asubuhi, lakini walinzi wanne walizuia waandishi kuingia kwenye chumba cha Mahakama.

Kabla ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa, walinzi hao walionekana wakizunguka eneo la Mahakama na muda ulipofika, walisimama mlangoni na kuzuia waandishi kwa madai kuwa kesi hiyo haiwahusu.

Mahojiano kati ya walinzi hao yalikuwa kama ifuatavyo:

Mlinzi: Mnakwenda wapi?
Waandishi: Tunaingia mahakamani
Mlinzi: Ninyi ni akina nani na mmeambiwa kuna Mahakama humu?
Waandishi: Sisi ni waandishi wa habari na hii ni Mahakama.
Mlinzi mwingine akasema: "Msiingie huku kesi hii haiwahusu" na kuweka mkono kwenye mlango wa chumba cha Mahakama kuzuia waandishi.
Mwinyi alimaliza kutoa ushahidi na kutoka kupitia mlango wa nyuma wa Mahakama saa 6.21 mchana na kuchukuliwa na gari namba T 914 BJT aina ya Toyota Land Cruiser lenye vioo vyeusi.

Mzee Mwinyi anakuwa Rais mstaafu wa pili kutinga mahakamani kutoa ushahidi katika kesi. Kabla yake, Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, alifika mahakamani hapo kutoa ushahidi katika kesi ya uhujumu uchumi iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu.

Tofauti ya kesi hizo mbili; Mwinyi yeye amekwenda kutoa ushahidi katika kesi inayomhusu yeye binafsi na iliyotokea wakati akiwa amestaafu, wakati Mkapa alikwenda kutoa ushahidi katika kesi iliyohusu utendaji wake akiwa Rais.

---
Habari via gazeti la HabariLeo