Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Saidi Meck Sadiki amesema ujenzi wa kituo
kipya cha mabasi yaendayo mikoani kinatarajiwa kujengwa eneo la Mbezi
Ruis.
Akizungumza na
NIPASHE, alisema serikali imeanza mkakati wa kuwahamisha wakazi wa eneo
hilo ili kupisha ujenzi wa kituo kipya cha mabasi kwani kituo cha Ubungo
kinachotumika hivi sasa, kitatumika kwa ajili ya mabasi yaendayo kwa
kasi (DART).
Alisema
kwa mabasi yanayofanya safari zake ukanda wa Kaskazini yatajengewa kituo
eneo la Boko na eneo la machimbo lililopo Kunduchi jijini Dar es
Salaam.
Kwa upande
wao Chama Cha Wamiliki wa Mabasi (TABOA), baada ya kutishia kutohama
katika Kituo cha Ubungo na kuunda tume ya watu watano ili kufikisha
malalamiko yao kwa Mkuu wa mkoa wamesema kuwa wamekubaliana na uamuzi
huo wa Serikali baada ya kushirikishwa kuhusu ujenzi huo.
Aidha,
Katibu wa chama hicho, Enea Mrutu, alisema baada ya kukutana na Mkuu wa
Mkoa na kufafanuliwa juu ya suala hilo, chama kimeridhia ujenzi huo na
hakutatokea vitisho vingine kuhusu kugoma kuhama Ubungo.
Hata
hivyo, Mrutu alisema pamoja na kituo kipya kujengwa eneo husika, bado
kutakuwepo na usumbufu mkubwa kwa wasafiri hasa wale waishio mbali na
kituo hicho.
--
via gazeti la Nipashe