Wednesday, September 26, 2012

MAJAMBAZI WAWADUNGA WATU SINDANO ZA SUMU MKOANI KILIMANJARO

WANANCHI wa kata tatu za Wilaya ya Moshi Vijijini, wamekumbwa na hofu kubwa inayofuatia kuibuka kwa vitendo vya ujambazi huku kukiwa na madai kuwa  majambazi hao hao, wanatumia sindano za sumu kuua watu.

Habari kutoka kata za Kilema Kusini, Kilema Kaskazini na Marangu zinadai kuwa mtandao wa majambazi hao wapatao 30, umekuwa ukilipiza kisasi kwa wananchi wanaojitokeza kutoa ushahidi polisi. Wananchi hao wamependekeza kutumika kwa sheria ya kuwaweka kizuizini watuhumiwa, ili kuepuka uwezekano wa  kuua watu.

Habari zilizozagaa katika Kijiji cha Makami Juu, zilidai kuwa usiku wa Septemba 11 mwaka huu,  majambazi walimvamia mfanyabiashara, Respich Ngowi na kumuua kwa kumdunga sindano ya sumu, “Waliiba kila kitu na wakamdunga sindano ya sumu, watu hawakuthubutu kutoka nje ya nyumba wakihofia kukatwa mapanga na kufuatiliwa na mtandao huo wa majambazi,”alidai mwananchi mmoja.

Wananchi hao walidai kuwa uchunguzi wa mwili wa marehemu uliofanywa na madaktari, ulithibitisha kuwa mfanyabiashara huyo alichomwa sindano mbili za sumu.

Mtandao huo ndio unaotuhumiwa kuilipua kwa petroli, nyumba ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Kiraracha, Andrew Lekule na kuteketeza mkewe na mtoto wao mdogo wa umri wa miaka mitano.

Mkazi mwingine wa Kijiji cha Kitowo huko Kilema, alidai kuwa mtandao huo ni kama umejitangazia “uhuru” kwa sababu unafanya uhalifu wakati wowote wanapojisikia kufanya hivyo, “Ukiuza nguruwe wanakufuata usiku na hata ukiuza mti wako wanakuja na mapanga wanataka pesa za mauzo. Hali si nzuri hata kidogo karibu kata nzima ya Kilema Kaskazini,”alidai.

Hata hivyo mkazi wa Kijiji cha Ruwa alilidokeza gazeti hili (MWANANCHI) kuwa pamoja na jitihada za polisi kukamata washukiwa lakini wananchi hawataki kutoa ushirikiano ikiwamo kuwatambua wahalifu, “Tatizo hapa ni wananchi ambao hawana mwamko wa ulinzi shirikishi, yaani mtu anavamia nyumbani na anapiga yowe la kuomba msaada, lakini  hakuna jirani anayetoka na kutoa msaada” alidai.

Mwananchi huyo ambaye naye hakupenda jina lake litajwe, alidai kuwa kama wananchi wangekuwa na umoja, wangeweza kusambaratisha mtandao huo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz, alikiri kuwapo kwa matukio ya ujambazi, lakini alisema tatizo ni wananchi wanaokataa kuwatambua washukiwa wala kutoa ushahidi.

...soma zaidi habari hii ya Daniel Mjema katika gazeti la Mwananchi