Friday, January 16, 2015

UKAWA WAANZA SAFARI YA URAIS 2015

Ukawa wakifafanua jambo
Wakati CCM ikisubiri Februari kufanya tathmini kuona kama baadhi ya wagombea wake wa urais wametekeleza masharti ya adhabu zao, washindani wao wa Ukawa, Jumanne ijayo watakutana kujadili mambo mbalimbali, ukiwamo mchakato wa kuwapata wagombea wake wa urais, ubunge na udiwani, imefahamika.
Tangu mwaka huu uanze zimekuwapo pilikapilika nyingi za kisiasa ndani ya vyama vya siasa na Jumanne iliyopita CCM ilifanya kikao cha Kamati Kuu mjini Zanzibar na kutoa maazimio yanayogusia mchakato huo lakini ikasita kutaja ratiba rasmi ya mchakato wa kuwapata wagombea wa CCM.
Wakati hali ikiwa hivyo, habari zilizopatikana na kuthibitishwa na baadhi ya viongozi wa Ukawa, umoja huo utakutana jijini Dar es Salaam Januari 20, ukiwa na ajenda mbalimbali kuhusu ushirikiano wao, likiwamo suala la kupata wagombea huku vikao vya ndani ya vyama vikitarajiwa mwishoni mwa mwezi huu.(P.T)
Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, James Mbatia alithibitisha jana kuwapo kwa kikao hicho Jumanne akisema kutakuwa na ajenda nyingine lakini: "Suala la kupata wagombea nalo huenda likajadiliwa. Kuhusu suala la mgombea urais wa Ukawa, linaweza kuwa sehemu ya mazungumzo lakini halipo kwenye ajenda."
Ajenda nyingine alizotaja ni mwongozo wa Ukawa, kura ya maoni ya Katiba, changamoto za uandikishaji wa daftari la wapigakura, hali ya uchumi na tathmini ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliomalizika Desemba mwaka jana. Mbatia, ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi alisema watajadili ajenda hizo ili kuhakikisha wanatafuta majibu ya changamoto zilizopo kwa sasa.
Kiongozi huyo pia alithibitisha taarifa kuwa kila chama ndani ya Ukawa kupitia vikao vyake kitateua majina ya wagombea ambao watashindanishwa ndani ya umoja huo, akisema kabla ya Machi, jina la mgombea urais ndani ya chama chake litakuwa limeshapendekezwa.
Awali, Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema vikao vya chama hicho vinavyotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu vitakuwa na ajenda ya uchaguzi vitakavyojadili mwelekeo wa uchaguzi huo kama kalenda yake inavyosema.
"Nadhani vikao hivyo ndiyo vitaanza kujadili ajenda ya uchaguzi ujao. Tulishatoa nafasi ya watu kujitokeza kwenye nafasi mbalimbali. Tukishapendekeza majina ya wagombea kwa baadaye ndiyo tutawapeleka ili kuchambuliwa kwa pamoja na kamati ya Ukawa.
"Mpaka sasa kamati ya Ukawa inaendelea na kazi yake tangu Oktoba mwaka jana ila inakuwa vigumu kwa wajumbe kujua kazi zote zinazofanywa na kamati hiyo kutokana na msingi wa majukumu yake."
Nyambabe alisema kamati hiyo imekuwa ikifanya kazi, ikijumuisha wajumbe wasiopungua watatu kutoka kila chama ili kufanya tathimini, kuchambua na kuratibu shughuli zote za uchaguzi.
Kuhusu kupata mwongozo wa Ukawa, Nyambabe alisema: "Namna ya kupata mgombea, ilani moja na mwelekeo, vinaweza kuonekana kuanzia Februari baada ya vyama kukaa vikao vyake."
Wakati Nyambabe akisema hayo, kumekuwa na taarifa katika vyombo vya habari kuwa CUF kimeshatangaza kumsimamisha Profesa Ibrahim Lipumba kuwania urais, ambazo hata hivyo, zimekanushwa na Naibu Katibu Mkuu wake Bara, Magdalena Sakaya.
Alisema kikao cha hivi karibuni ndani ya chama hicho kilikuwa na ajenda ya kutathimini Uchaguzi wa Serikali za Mitaa tu na hakukuwa na ajenda nyingine iliyojadiliwa. "Bado hatujapendekeza jina lolote," alisema Sakaya.
Hata hivyo, Sakaya alisema kikao kijacho cha wenyeviti wa Ukawa hakitakuwa na mamlaka yoyote ya kuamua au kupitisha jambo bila kupata baraka za viongozi wa Baraza la Uongozi Taifa kutoka kila chama.
"Kikao hicho sijafahamu ajenda yake lakini ifahamike tu kwamba, ndani ya Ukawa kuna vikao vitatu; kikao cha maofisa, kikao cha makatibu na kikao cha wenyeviti na hufanyika kwa kuzingatia ratiba zake," alisema na kuongeza:
"Kwa hivyo utaratibu wa mgombea hauwezi kupatikana kwa sasa kwani hakuna chama ambacho kimejadili ajenda yoyote au kupitisha majina ya wagombea wake."
Sakaya alisema kabla ya kujadiliwa ndani ya Ukawa, vikao vya mabaraza na kamati kuu za vyama husika vitakuwa vimeshiriki kuchambua na kupitisha majina ya wagombea wake wanaokidhi vigezo.
"Baada ya hapo ndipo majina yatafikishwa Ukawa na kamati itachambua wanaoweza kusimama kwa niaba ya Ukawa kutokana na tathimini yao watakayokuwa wameipata," alisema na kuongeza:
"Kwa upande wa CUF, kalenda yetu inaonyesha kuwa na vikao mwishoni mwa mwezi huu. Nadhani kutakuwa na mwelekeo juu ya uchaguzi ujao." Viongozi wa juu wa Chadema jana hawakupatikana kuzungumzia suala hilo, lakini Ofisa Habari wake, Tumaini Makene alisema kwa sasa chama hicho hakijafikiria kuwa na vikao vyenye ajenda ya kuangalia jina litakalopitishwa kwa ajili ya kuingia Ukawa...
"Bado kabisa kuhusu suala la kujadili mgombea urais wa Ukawa, hatujafikiria hilo ila kinachotuumiza akili kwa sasa ni kero za daftari la wapigakura na kuwapo kwa tume isiyokuwa huru ya uchaguzi. Ratiba ya ajenda hiyo ikitoka tutajulishana," alisema Makene.
Chanzo:Mwananchi

No comments:

Post a Comment