Thursday, May 22, 2014

MAKUBWA YAFICHUKA KIFO CHA ADAM KUAMBIANA, YADAIWA ALIJIUA. SOMA HAPA

    

IMEVUJA! Siku chache baada ya kifo cha mwongozaji na mwigizaji wa filamu Bongo, Adam Philip Kuambiana, daktari mkubwa wa mastaa ameibuka na kudai marehemu alijiua mwenyewe.

Kwa mujibu wa daktari huyo ambaye hakupenda jina lake lichorwe gazetini kutokana na maadili ya taaluma yao kuficha siri ya mgonjwa, siku moja kabla ya kifo (Ijumaa ya Mei 16, mwaka huu), marehemu alimpigia simu na kumwambia amekunywa dawa za malaria aina ya Fansidar lakini pia amekunywa pombe.

ILIVYOKUWA
Daktari huyo alieleza kuwa, marehemu alimpigia simu kumuomba ushauri juu ya nini cha kufanya na kama kuna madhara yoyote juu ya pombe hizo na dawa alizokunywa.

“Aliniuliza kama kuna madhara yoyote ambayo anaweza kuyapata kwa kuwa alikuwa amekunywa fansidar kwa ajili ya malaria kisha akapata kiu ya bia na kuamua kunywa,” alisema daktari huyo.

AMSHAURI KWENDA HOSPITALI
Akizidi kuzungumzia tukio hilo, daktari alikwenda mbele kwa kusema licha ya msanii huyo kuwa na ‘masikhala’ mara kwa mara, lakini kwa kuwa alimwambia jambo ambalo linahusu uhai wake, alimshauri kwenda hospitali iliyo karibu ili akaonane na daktari kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kutoa sumu kwani kitaalam mtu anapokunywa pombe akiwa amemeza dawa za aina hiyo vyote hugeuka kuwa sumu.

Alisema kutokana na jinsi alivyozidi kumsimulia hali aliyonayo, aliamini kwamba marehemu alikuwa anamaanisha alichokuwa akikisema hivyo ikabidi amsisitize kuwahi hospitali haraka.

“Nilimwambia awahi hospitalini haraka kwani nilijua fansidar ni kali na si dawa ya kufanyia mchezo. Lakini kesho yake nilipopata taarifa za kifo chake niliumia sana japokuwa nilijua amejiua kwa kuchangaya fansidar na bia maana mchanganyiko wa sumu yake mwilini ni mkali sana,” alisema daktari huyo huku akisisitiza kusitiriwa kwa jina lake.

MAZINGIRA YA KIFO
Kwa mujibu wa mtu ambaye alikuwa karibu na Kuambiana siku ya tukio ambaye naye hakutaka kutajwa jina gazetini, marehemu asingekufa ghafla kama tatizo alilokuwa nalo lingekuwa la vidonda vya tumbo ambavyo vilikuwa vikimsumbua kwa muda mrefu.

“Siku ile marehemu alikuwa na pesa, alikunywa sana pombe kutoka asubuhi mpaka usiku mwingi, alikuwa anakula kila anapojisikia sasa hatuelewi ni kitu gani kilitokea maana haiwezekani mtu akutwe anaendesha na kutapika damu pasipo kuwa na sumu mwilini,” alisema mtu huyo.

DAKTARI AWAASA MASTAA
Katika hatua nyingine, daktari huyo aliwashauri mastaa wengine kuwa makini kwani mara kadhaa amepata kesi za namna hiyo ambapo wanakunywa pombe vilabuni usiku huku wakiwa katika dozi ya ugonjwa fulani.
Source:GPL

No comments:

Post a Comment