Tuesday, January 7, 2014

DAKTARI NGULI WA KUTOA MIMBA ANASWA DAR...!SOMA ZAIDI HAPA...


MWAKA umeanza, mambo mapya pia yapo! Oparesheni Fichua Maovu ‘OFM’ ya Global Publishers imeingia kazini kwa kasi zaidi. Safari hii imemnasa daktari anayejulikana kwa jina moja la Mambo maarufu sana kwa jina la Dokta Mambo katika jaribio linalodaiwa kuwa ni la utoaji mimba.


Tukio hilo lilitokea katika zahanati yake (jina lipo) iliyopo Kawe jijini Dar es Salaam ambapo daktari huyo anayejulikana sana na wateja wake, hasa akina mama alipoingiliwa na OFM wakishirikiana na polisi baada ya kumuwekea mtego wa mbinu za kishushushu.
MALALAMIKO YA AWALI
Mwishoni mwa Desemba, mwaka jana, mtu mmoja (jina lipo) alituma ujumbe mfupi wa maneno (SMS) kwenda OFM akimlalamikia dokta huyo kwamba amekuwa na mchezo wa kutoa mimba wanawake wakiwemo mabinti wa shule, kitendo alichodai haoni kama ni sawa.

“Naitwa….(jina lipo), nilikuwa naishi Kawe lakini kwa sasa nimehamia Mbezi (hakusema Mbezi gani). Kama hapo ni OFM (Oparesheni Fichua Maovu) naomba mumshughulikie daktari mmoja anaitwa Dokta Mambo wa Kawe. Huyu daktari jamani amekuwa na tabia ya kutoa mimba wanawake hata wasio na matatizo.
“Ninavyojua mimi hakuna hospitali inayoruhusiwa kutoa mimba Tanzania, labda pale ambapo itathibitika kwamba mjamzito ana kifafa, kwa hiyo hatari inakuwepo ya kumpoteza mama au mtoto tumboni ndiyo mimba hutolewa. Wananchi wa Kawe wamekilalamikia kitendo hicho hadi wamechoka. Polisi Kawe wamemshindwa,” alisema raia mwema huyo.
OFM YAANZA KAZI
Baada ya kupokea tuhuma hizo, OFM ilijipanga na kuingia kazini. Ilimwandaa paparazi wa kike na kumtengenezea ujauzito wa bandia na paparazi wa kiume ambaye ni mchumba wake (wa bandia) ili kwenda naye kwa Dokta Mambo kuona kama kweli anajihusisha na kazi hiyo au la!

JUMANNE, DESEMBA 31, 2013
Ilikuwa Jumanne ya Desemba 31, 2013, OFM na paparazi huyo walitia timu kwenye zahanati hiyo na kukutana na dokta huyo ambaye al
ikubali kumtoa ujauzito paparazi huyo.
‘Mchumba’ wa paparazi huyo alimwambia dokta kwamba wamekubaliana kuitoa mimba hiyo kwa sababu ya hali ya uchumba, daktari akasema haina shida.

AWEKA MASHARTI MAGUMU   
Katika hali ambayo OFM hawakuitarajia, daktari huyo alisema kwa kawaida kabla hajamchoropoa mimba mteja wake lazima aipime kwanza ili kujua ina muda gani.
Zoezi hilo lilikuwa gumu kwa OFM kwa sababu paparazi huyo hakuwa na ujauzito. Ilibidi ‘wateja’ hao waondoke kwa kisingizio kwamba wanakwenda kujipanga kwa fedha aliyoitaka ambayo ni shilingi laki moja na kwamba wangerudi siku iliyofuata (Jumatano).

OFM WAJIPANGA UPYA
‘Wachumba’ hao waliondoka na kuungana na Timu ya OFM ambayo ilikuwa mahali imekaa mkao wa mtego. Baada ya kupata simulizi za ndani ya zahanati hiyo, OFM ilirejea ofisini na kumweleza kamanda mkuu wake ambaye alikaa na timu hiyo na kupanga mpango mpya.

“Bosi, Dokta Mambo ameshakubali, lakini sera zake ni kwamba hawezi kumtoa mimba mjamzito hadi ampime kwanza na kujua ina miezi mingapi. Sasa huyu (paparazi) hana ujauzito, tungekubali ampime tungeumbuka, tukamwambia tunakwenda kusaka fedha kwanza,” OFM  mmoja alimwambia kamanda mkuu.
OFM YATUMWA MTAANI KUSAKA MWENYE MIMBA YA UKWELI
Kamanda Mkuu wa OFM (jina lipo) aliagiza timu yake kuingia mtaani ili kumsaka mwanamke mwenye mimba ya ukweli ambaye ndiye angekuwa na sifa za kutolewa ujauzito na daktari huyo.
Hayo yote yalifanyika baada ya pia uchunguzi wa kina kufanyika maeneo ya Kawe kuhusu tabia ya daktari huyo na kudaiwa kuwa, hawezi kuacha ‘kamchezo hako ka siku nyingi’.

Mjamzito wa kweli alipatikana (jina lipo), akiwa na mimba ya miezi mitatu.  Akashirikishwa katika zoezi hilo ambapo hata yeye aliumia kusikia kwamba kuna daktari anayetoa mimba wanawake hata wale ambao hawana sababu za kufanya hivyo kama sheria za utabibu zinavyotaka.
WATINGA POLISI KAWE
Baada ya kupatikana kwa mjamzito huyo, OFM ilimchukua hadi Kituo cha Polisi Kawe, Dar es Salaam na kuwaambia wahusika kuhusu tabia ya daktari huyo inayolalamikiwa na watu ili ikibidi watoe askari kwa kuungana na OFM kwenda kumtia nguvuni.

POLISI KAWE WAONESHA ‘MAAJABU’
Katika hali ya kushangaza, polisi wa kituo hicho, awali waliwataka OFM watoke nje ili wajadili wao. Baadaye waliwaita na kusema kwamba hawawezi kutoa polisi, kama ishu ni daktari huyo kulalamikiwa na watu, watamwita na kumkanya aache mchezo huo!

“Hatuwezi kushirikiana nanyi katika hilo zoezi, kama ni kweli kuna hayo maneno ya watu, sisi tutamwita tumuonye aache mara moja,” alisema mmoja wa askari wa Kituo cha Kawe.
Katika hali iliyoshangaza zaidi, polisi hao waliwataka waandishi wote walio kwenye msafara kuandika maelezo ya malalamiko kuhusu daktari huyo kwenye kitabu cha ripoti kituoni hapo (Report Book ‘RB’).
Maelezo yaliandikwa. Jina……, umri…., makazi…., kazi…., dini….. na aina ya malalamiko. Baada ya hapo wakatakiwa kuondoka zao.

OFM WARUDI KWA DOKTA MAMBO
Januari 3, 2014, OFM wakiwa na mjamzito wa kweli  walikwenda kwa dokta huyo ambapo kama ilivyo utaratibu wake, alimpima kwanza na kutoa majibu kwamba ana mimba ya miezi 3 na wiki mbili, akasema ni kubwa sana, hivyo zinatakiwa shilingi 160,000.

Hata hivyo, mchumba mtu alisema hana kiasi hicho cha pesa. Ikatokea vuta nikuvute hadi kufikia shilingi 100,000. Ikumbukwe kwamba, mpaka hapo Dokta Mambo hakuwa anajua kwamba mchezo wa pili ni uleule wa kwanza.
“Basi dokta tunaomba tuje kesho na hiyo laki moja,” mchumba mtu alimwambia daktari huyo ambaye alikubali huku na yeye akiomba kuwa, hiyo kesho iwe saa kumi na moja jioni.
OFM, POLISI, MJAMZITO NA MCHUMBA’KE
Kesho yake ilifika, OFM ikiwa na mjamzito huyo akiwa na mchumba’ake walikwenda maeneo ya Kawe jirani na zahanati ya Dokta Mambo kujaribu kupanga namna ya kufanikisha oparesheni hiyo.

Bado tatizo lilikuwa uwepo wa polisi baada ya kubaniwa na wale wa Kawe. Mungu si Athumani, wakiwa wanashangaashangaa eneo, ilipita pikipiki ya askari wa doria ‘Tigo’ na mara moja OFM ikawasimamisha.
Bila kupoteza muda, OFM waliwaeleza polisi wale mchezo mzima ulivyokuwa na kwamba walihitaji msaada wao ili kufanikisha zoezi hilo, walikubali bila kinyongo na mara moja wakaongozana hadi eneo la tukio.
OFM mmoja kati yao aliingia ndani ya zahanati hiyo akijifanya amekwenda kupima malaria, wale polisi wawili na OFM wengine walikaa mafichoni kutega mingo, wachumba nao waliingia mpaka kwa dokta wakiwa na kitita cha shilingi laki moja mkononi.
MJAMZITO APELEKWA CHUMBA CHA KAZI
Baada ya kuwapokea na kutoa kiasi hicho cha pesa, mjamzito huyo alipelekwa chumba kinachodaiwa ni cha kutolea mimba huku mchumba mtu akikaa kwenye fomu kusubiri matokeo.

UTAALAM WA OFM
Kilikuwa kipindi kinachotaka mawasiliano ya hali ya juu, OFM ikitambua kuwa kosa moja goli moja, walikuwa makini kwa mawasiliano. Mjamzito chumbani kumwambia mchumba wake kwenye fomu, naye kuwaambia OFM wa nje hatua kwa hatua.

Katika mazingira hayo, hakuna OFM aliyetakiwa kupokea simu wala kutuma meseji kwa mtu asiyehusiana na kazi hiyo.
TUKIO LANASWA
Ilikuwa wakati daktari huyo akiwa na glovsi mikononi, mjamzito wa kweli akiwa kitandani na nesi mmoja wa kumsaidia daktari wakiwa ndani ya chumba, ndipo OFM na polisi walipovamia na kunasa tukio ambalo lilionekana dhahiri kwamba lilikuwa jaribio la kutoa mimba.

Hapo ndipo Dokta Mambo alipogundua kuwa kumbe ‘kazi’ aliyopewa ilikuwa feki na wale walikuwa makamanda wa OFM wakishirikiana na polisi waaminifu, wazalendo na wanaopenda kazi yao sawasawa.
KWA NINI?
Lilikuwa jaribio la kutoa mimba kwa sababu, ndani ya chumba zilikutwa zana za shughuli hiyo huku mjamzito akiwa kitandani tayari kwa kufanyiwa mchakato.

Huku OFM wakimpiga picha (zipo za kumwaga kwenye maktaba yetu – ukitaka kuziona njoo Bamaga), askari nao wakichunguza mazingira zaidi na kukamata vifaa, daktari huyo alinywea huku msaidizi wake akitokwa machozi.
POLISI WAMWINGIZA NDANI YA GARI
Zoezi hilo lilikamilika kwa daktari huyo kuchukuliwa na askari hao ambao walikodi gari, mmoja akawa na dokta garini akiwa na vifaa vyake chini ya ulinzi, mwingine akiwafuata kwa nyuma na pikipiki.

Askari hao, waliwaeleza OFM kuwa wataitwa Kituo cha Polisi Oysterbay kwa ajili ya kuandika maelezo.
Risasi Mchanganyiko lilimtafuta kwa njia ya simu Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, ACP Camillius Wambura ili kujua kama suala hilo limefika mezani kwake, lakini simu yake haikupatikana muda wote ilipopigwa.

Hata lilipomtafuta Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, CP Suleiman Kova ili limsimulie mchezo mzima ulivyokuwa, naye hakupatikana hadi tulipokwenda mitamboni.
Bado tunaendelea kuwatafuta viongozi wa polisi na ukweli wa kina kuhusu namna ishu hiyo inavyoendelea, tunawajulisha katika matoleo yetu yanayofuata

No comments:

Post a Comment