Friday, March 15, 2013

Watu wanne wafikishwa mahakamani wakituhumiwa kumuua kwa maksudi John Mwankenja aliyekuwa Diwani wa Kata ya Kiwira(CCM) na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe..



 Marehemu John Mwankenja aliyekuwa Diwani wa Kata ya Kiwira(CCM) na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe..



Watu wanne wamefikishwa katika mahakama kuu kanda ya Mbeya wakituhumiwa  kumuua kwa maksudi John Mwankenja aliyekuwa Diwani wa Kata ya Kiwira(CCM) na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe..
Mwendesha mashtaka wa Serikali Basilius Namkambe aliaambia Mahakama hiyo Mbele ya Jaji Samweli Karua kuwa watuhumiwa hao walitenda kosa hilo Mei 15,2011 katika Kijiji cha Mpandapanda kata ya Kiwira Wilayani Rungwe kinyume na kifungu cha 196(16) kilichofanyiwa marekebisho Mwaka 2002.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Hakimu Mwakalinga ambaye ndiye mtuhumiwa namba moja katika kesi hiyo akiwa na Daudi Mwasipesya,Obote Mwanyimbili na Kelvin Maurus Myovela ambao wanatuhumiwa kumuua John Mwankenja aliyekuwa Diwani wa Kata ya Kiwira(CCM) na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe.
Awali baada ya kupandishwa kizimbani watuhumiwa kujibu kesi inayowakabili yenye namba 31/2012 walimkataa Wakili aliyejulikana kwa jina moja laMwakabubu aliyekuwa ameteuliwa kwa ajili ya kuwatetea kwa madai kuwa hawana imani naye kutokana na mwenendo wa kesi alizosimamia.
“Mtukufu Jaji kabla ya kesi yetu haijaanza kusikilizwa tunaomba kubadilishiwa Wakili kwa sababu huyu Mwakabubu hana uwezo na tumeona kesi ndogo tu anababaika na kesi yetu ni kubwa tunaona wazi kabisa kuwa hataweza kututetea” alisema Mwakalinga Mshitakiwa namba moja.
Kufuatia ombi hilo Jaji Karua alikubaliana nao ambapo alimteua Wakili mwingine ambaye ni Sambwee Shitambala ambaye walimkubali kabla hajawaongezea wakili mwingine ili asaidiane na Shitambala ambapo alimtaja Wakili Zakia Selemani.
Akisoma mashtaka yao Mwendesha mashtaka wa Serikali Basilius Namkambe  aliiambia mahakama hiyo kuwa mnamo tarehe 19, Mei 2011 majira ya jioni marehemu akiwa anatokea Mbeya mjini akirudinyumbani kwake Kiwira Wilayani Rungwe alifika Nyumbani akiwa na gari lenye namba za usajili T 127ACZ Nissan (Double cabin).
Namkambe aliongeza kuwa baada ya kufika nyumbani kwake alipiga honi ya gari kwa ajili ya kuomba kufunguliwa geti la mlango ambapo baada ya kusikia honi hiyo alitoka Mjomba wake ambaye baada ya kumfungulia aliambiwa ashushe Kuku aliyokuwa amewabeba nyuma ya gari yake.
Alisema kabla ya mjomba wa Marehemu hajaanza kushusha kuku kwenye gari alitokea mshitakiwa namba moja akiwa na siraha ambapo alimwamuru asifanye lolote ndipo akaanza kufyatua risasi akimwelekezea marehemu kisha kumuuana kutoweka kusiko julikana.
Akijibu tuhuma hizo Wakili wa Utetezi Shitambala na Zakia walikana washtakiwa hao kuhusika na matukio hayo pamoja na baadhi ya vielelezo vilivyotolewa na upande wa mashtaka kuthibitisha kuhusika kwa wateja wao.
Walisema mtuhumiwa wa kwanza hakuwepo Wilayani Rungwe siku ya tukio ambapo walisema atakuwa na mashahidi ambao watathibitisha kwamba hakuhusika ambao waliwataja kuwa ni pamoja na yeye mwenyewe, Askari Magereza wawili wa gereza la Tukuyu Wilayani Rungwe waliotajwa kwa jina moja moja la Hereda na Green.
Wengine ni Padeso Mwakipesile, Aneth Siandene Kalinga na Jumanne Mwakisole huku washtakiwa namba mbili, tatu na nne ambao hawatakuwa na mashahidi ambapo watasimama wao wenyewe kujitetea.
Namkambe aliiambai mahakama hiyo kuwa upande wa mashtaka utakuwa na mashahidi zaidi ya 15 ambao aliwataja kuwa ni pamoja na Sofia Fungameza, Weston Gilbert,Magdalena Mgawe, Musa Jackson, Issa Mwaipopo, Teresia Ludovick na Williamu Mtanga.
Wengine ni askari Polisi Mwenye namba D2385 Sajent Michael wa Tukuyu, Inspekta Isaya Bwile wa Tukuyu, David Paul kutoka makao makuu ya Polisi Dar Es Salaam, Twaha kutoka kitengo cha Upelelezi makao makuu ya Polisi Dar Es Salaam, Haruna kutoka Polisi Tukuyu na WP3433 Agnes wa polisi Tukuyu.
Namkambe aliwataja mashahidi wengine katika kesi hiyo kuwa ni pamoja na aliyekuwa Mkuu wa upelezi (RCO) Mkoa wa Mbeya aliyehamishiwa makao makuu SSP Anacletus Malindisa, John Mayunga na Dk. D Z Matata kutoka ofisi ya Mkemia mkuu wa Serikali.
Jaji Karua aliahirisha kesi hiyo hadi hapo itakapopangwa tena kwa ajili ya kuendelea na kuwasilikiza mashahidi kutoka upande wa mashtaka baada ya kuambia mahakama kuwa upelelezi umekamilika na mashahidi wote wako tayari.
Na Venance Matinya, Mbeya.

No comments:

Post a Comment