Imeandikwa na Happiness Katabazi via blog
MAHAKAMA ya Hakimu
Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imesema kuwa Aprili 18 mwaka huu, itaoa
hukumu ya kesi ya uchochezi wizi wa malighafi za Silingi milioni 59
inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa
Ponda na wenzake 49.
Hakimu Mkazi Victoria Nongwa aliyasema hayo
saa kumi alasiri muda mfupi baada ya mashahidi watano wa upande wa
utetezi waliopanda wote kizimbani kutoa utetezi na hivyo kufanya upande
wa utetezi weleta mashahidi 52.
Hakimu Nongwa alizitaka pande
mbili katika kesi hiyo kuwasilisha kwa maandishi majumuisho ya mwisho ya
kesi hiyo Aprili 3 mwaka huu, na kwamba kesi hiyo itatajwa Aprili 4.
Kabla
ya kuyasema hayo Ponda jana alipanda kizimbani na kuanza kutoa
kujitetea ambapo alidai kuwa ni kweli yeye ndiye aliyetoa maagizo kwa
maimau wa misikiti wawatangazie waumini wao ili waje kwenye kiwanja cha
Chang’ombe Markas kwaajili ya kuja kuongeza nguvu ya kujenga msikiti wa
muda katika kiwanja hicho.
Itakumbukwa kuwa mashahidi watatu wa
kesi hiyo ya uchochezi na wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh.milioni
59 inayomkabili Ponda na wenzake 49 jumla ya mashahidi wa tatu ambao ni
viongozi wa Bakwata na mkurugenzi wa kampuni ya Agritanza, walitoa
ushahidi wao na kusema kuwa awali kiwanja hicho kilikuwa kikimilikiwa na
Bakwata ambayo ndiyo yenye dhamana ya kumiliki mali zote za waislamu
lakini Bakwata ikaamua kuipatia kiwanja hicho Agritanza na Agritanza
ikaipatia Bakwata kiwanja kikubwa kilichopo Kisarawe kwahiyona kusema
kuwa kiwanja cha Markas siyo mali ya waislamu wala Bakwata lakini
washitakiwa katika utetezi wao wanadai kiwanja hicho ni mali ya
waislamu.
Sheikh Ponda aliyekuwa akiongozwa kutoa utetezi wake na
wakili wake Juma Nassor na Njama mbele ya Hakimu Mkazi Victoria Nongwa
alieleza ni yeye ndiye aliyetoa maelekezo hayo ya kuwataka waislamu
wote wafike katika eneo hilo ili wajenge msikiti wa muda na kwamba
waislamu hao waliitikia wito na kwamba kuanzia asubuhi ya saa moja hadi
saa 12 jioni ya Oktoba 12-14 yeye na waislamu hao walikuwa wakijenga
msikiti huo ndani ya kiwanja hicho ambacho ni mali ya waislamu.
“Kiwanja
hicho ni mali ya waislamu na kiwanja hicho tulipewa sisi waislamu na
serikali ya Misri tena wakati huo waislamu wote tulikuwa chini ya East
Africa Muslim Welfare,lakini baadae taasisi hiyo ilifutwa na serikali
ndiyo ikaanzishwa Bakwata…kwahiyo kufutwa kwa taasisi ile hakumaanishi
mali zilizokuwa chini ya taasisi zake nazo zimefutwa,kinachofanyika pale
ni majukumu ya taasisi yale yanakuwa yamesimama na mali zake zinabaki
kuwa ni za wanachama wake wa taasisi hiyo iliyofutwa ”alidai Sheikh
Ponda
Hata hivyo alikanusha mashitaka yote yanayomkabili na
kusema hafahamu ni kwanini upande wa Jamhuri umemfungulia mashitaka hayo
kwa sababu hata hilo kosa la wizi wa malighafi, mahakama ilipaswa
ihamie kwenye eneo la tukio iende ikashuhudie kama wale Waislam
niliokuwa nao walichukua malighafi za kampuni ya Agritanza ili kujengea
msikiti wa muda.
Akielezea jinsi alivyokamatwa na askari, Ponda
alidai Oktoba 16 mwaka jana, saa nne kasoro wakati akiingia ndani ya
msikiti wa Tungi uliopo Temeke , kabla ya kuingia ndani alisikia sauti
ya mtu ikimuita na mtu huyo alikuwa ndani ya gari, akawataka watu hao
wamfuate nyuma.
“Nilipoingia msikitini nikasikia sauti ya magari
nikatazama nikaona magari matatu aina ya Land Cruiser yana askari wa
kikosi cha FFU wakiwa na silaha na mabomu na wale askari walingia ndani
ya msikiti wakiwa wamevaa viatu wakanivamia na kuniangusha chini,
wakanitoa ndani ya msikiti kwa mtindo wa kuniteka nyara na kunikimbiza
kwenye gari lao kwa kasi,”alidai Sheikh Ponda.
Aliendelea kudai
kuwa walimepeleka katika kituo cha polisi Chang’ombe na, “wakanieleza
kosa langu na wakaniambia mimi siyo raia wa Tanzania, ni kwa nini
nisiende kufanya vurugu Burundi? Mi nikawaambia ni raia wa Tanzania,”
alidai Ponda.
Akijibu maswali ya wakili Mwandamizi wa Serikali
Tumaini Kweka kuwa hakuona ni kosa kwa yeye kuita Waislam waende kujenga
msikiti wa muda katika eneo lile ambalo si mali ya Waislam, Ponda
alijibu kuwa, ‘Sikiliza Kweka, mimi nimeanza mijadala tangu enzi
Serikali ya rais Julius Nyerere, kwa hiyo nina uzoefu na huo siyo
uchochezi,” alidai Ponda.
Kwa upande wake mshitakiwa wa tano,
Mkadamu Abdallah akijitetea yeye alidai kuwa hafahamu hicho kiwanja
kiliuzwa kwa nani, na wala hajawai kutoa maelezo polisi na hafahamu kama
Ponda alienda kwa Mufti wa Tanzania, Sheikh Simba kumuuliza ikiwa
kiwanja hicho kimeuzwa.
Hata hivyo, wakili Kweka alipomtaka Mkadamu arejee maelezo yake aliyoyatoa polisi ambayo yamepokelewa mahakamani kama kielelezo.
Ndani
ya maelezo hayo, Mkadamu alikiri kufahamu kuwa kiwanja kile kimeuzwa
kwa Agritanza na BAKWATA na kwamba yeye na Waislam wenzake walienda
katika kiwanja hicho na kuanza kujenga msikiti wa muda.
Mkadamu aliishia kudai kuwa maelezo hayo si yake.
Oktoba
18 mwaka jana, kesi hiyo ilifunguliwa mahakamani hapa kwa mara ya
kwanza ambapo washitakiwa wanakabiliwa na jumla ya makosa matano ambayo
ni kula njama kutenda kosa, kuingia kwa jinai, kujimilikisha kwa nguvu
kiwanja hicho na wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh. milioni 59 na
uchochezi.
No comments:
Post a Comment