Wednesday, March 6, 2013

AKUTWA NA COCAIN KILO 6,, NA MWANAFUNZI UDSM AKAMATWA KWA KUMTEKA MTOTO

MTU mmoja anayesadikiwa kuwa mfanyabiashara wa dawa za kulevya, amekamatwa na Polisi mkoani Kilimanjaro katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) akiwa na kilo 6 za unga wa Cocaine.

Mtu huyo aliyefahamika kwa jina la Iddi Hassan Chumu (34), alikamatwa uwanjani hapo Februari 2, majira ya saa 3:45 jioni, akiwa anataka kusafiri kuelekea Hungary kwa kutumia ndege ya Qatar Airways kupitia Doha.

Taarifa hizo zinasema kuwa Chumu alikuwa ameficha unga huo ambao kwa sasa umepelekwa kwa Mkemia Mkuu kwa ajili ya vipimo zaidi.

Chumu anadaiwa ni mkazi wa Sinza jijini Dar es Salaam, ambapo kwa sasa anashikiliwa na Polisi huku majibu yakisubiriwa kutoka ofisi ya Mkemia Mkuu kuthibitisha kama kweli unga aliokamatwa nao ni dawa za kulevya au la.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz, alisema mtu huyo alikamatwa unga huo ukiwa umehifadhiwa chini ya begi lake la nguo, lakini mpaka sasa haijathibitika kuwa ni unga wa aina gani.

Kamanda Boaz alisema wapo watu wanaofikiri kuwa Kilimanjaro ni kivuko cha dawa za kulevya na kusisitiza kuwa Jeshi la Polisi liko macho na kamwe hataruhusu heshima ya mkoa huo kuchafuliwa na watu wachache.

“Kuna watu wanadhani kuwa hapa kwetu ni uchochoro wa kupitisha madawa ya kulevya na uchafu wa aina yoyote ile, hapa sio kivuko na kamwe hatutaruhusu hilo. Chumu kwa sasa yuko chini ya mkono wa Polisi na uchunguzi ukimalizika atafikishwa mahakamani,” alisema Boaz.

Wakati huohuo, Jeshi la Polisi mkoani hapa limewakamata watu wawili wanaodaiwa kumteka mtoto kwa madai ya kupata fidia kutoka kwa wazazi wa mtoto huyo. Taarifa hizo zinasema kuwa mtoto huyo alitoweka nyumbani kwa bibi yake Februari 27, majira ya saa 4 asubuhi na kwamba baada ya kufanyika kwa operesheni maalumu kutoka kwa kikosi maalum cha Jeshi la Polisi, alikutwa akiwa mikononi mwa mateka hao.

“Baada ya kupata taarifa, tuliunda timu maalumu na kuwapata watekaji wakiwa wilayani Rombo, mtego wetu ulinasa na kumkamata Nicholaus Lyimo akiwa amejificha katika Kijiji cha Mashimba, Useri Rombo akiwa na mtoto machakani, tulivyompekua tulikuta vyeti vyake vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kisu,” alisema Boaz.

---
Habari imeandikwa na Fadhili Athumani, Moshi via gazeti la MTANZANIA


No comments:

Post a Comment