Saturday, October 13, 2012

SERIKALI YASHITAKIWA NA LHRC KWENYE MAHAKAMA YA KIMATAIFA HUKO ICC KUTOKANA NA VIFO VYA UTATA VINAVYO ICHAFUA SERIKALI

MAUAJI ya mwandishi wa habari wa kituo cha runinga cha Channel Ten, Daudi Mwangosi, na ya raia wengine yamezidi kuichafua Serikali ya Tanzania, na sasa imefunguliwa mashitaka katika Mahakama ya Uhalifu ya Kimataifa (ICC) iliyoko The Hague, Uholanzi.

Mbali ya mashitaka hayo yaliyopelekwa huko tangu Septemba 28, mwaka huu, Tanzania pia imeshitakiwa kwenye Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu.

Mashtaka hayo yalifunguliwa na Kituo cha Haki za Binadamu, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wake, Hellen Kijo-Bisimba, alisema wamezitaka mamlaka hizo za kimataifa kufanya uchunguzi na kuichukulia hatua stahiki za kisheria Serikali ya Tanzania.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimechukua hatua hiyo kutokana na kuongezeka kwa mauaji ya raia wakiwa katika mikono ya vyombo vya dola, huku serikali ikigwaya kuwachukulia hatua za kisheria waliohusika.

Pamoja na hatua ya kushtakiwa kwa serikali katika mamlaka hizo za dunia, Bisimba alisema bado wanataka kuona viongozi wote wa serikali na vyombo vya dola waliohusika kwa namna yoyote na mauaji ya Mwangosi na raia wengine wakiwajibishwa.

Bisimba alisema hawaoni sababu za viongozi hao kutojiuzulu ama kuachishwa kazi na kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo.

Aidha, mkurugenzi huyo aliitaka serikali kuacha propaganda zinazotaka kuchochea vurugu katika taifa ambazo hazina tija na kutaka itambue kuwa sasa ni wakati wa mfumo wa vyama vingi, hivyo ni vyema ikaacha kutumia vyombo vya dola katika kuleta chuki na mafarakano katika jamii yanayohatarisha usalama na amani ya Watanzania.

---
Ni sehemu ya habari kwenye gazeti la Tanzania Daima.
---

Sehemu ya habari kwenye gazeti la Mwananchi iliyoandikwa na  Ibrahim Yamola na Raymond Kaminyoge inasema:

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dkt. Helen Kijo-Bisimba alisema kuanzia Januari hadi Septemba mwaka huu, jumla ya watu 24 wameuawa na watendaji wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Dkt. Kijo-Bisimba Alisema:

“Tumepeleka mashtaka 24 ICC tangu Septemba 28 mwaka huu, ambayo yanahitajika kufanyiwa uchunguzi na kuchukua hatua kali dhidi ya Serikali ya Tanzania ambayo imekuwa ikiwalinda viongozi wake wanaokiuka haki za binadamu,” alisema Dkt. Bisimba.

“Tunatarajia kuona uwajibikaji wa viongozi wote wa Serikali na vyombo vya dola waliohusika kwa njia yoyote ile. Hatua hizo au uwajibikaji huo ni pamoja na kujiuzulu, kuachishwa kazi na kufikishwa Mahakamani, ” alisema.

Taarifa ya Kamati ya Dkt. Nchimbi... “LHRC hakijashangazwa sana pale taarifa hiyo ilipoonyesha wazi nia ya kuwalinda watuhumiwa kwa kuwa Serikali yetu bado haijajenga mfumo wa kujichunguza na kujiwajibisha yenyewe.” “Serikali imeudhihirishia umma kuwa haikuwa na nia ya dhati ya kuchunguza suala la mauaji yaliyofanywa na Jeshi la Polisi, bali ilikuwa na lengo la kulisafisha Jeshi la Polisi na kuwalinda maofisa wake.”

Dk Bisimba alisema tangu mwaka 2001 hadi sasa, kituo hicho kimekuwa kikifuatilia kwa karibu matukio mbalimbali ya mauaji yanayoendelea kufanywa na vyombo vya dola na hakuna hatua zinazochukuliwa dhidi ya wahusika.


Kauli za Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mawakili

Akizungumzia suala hilo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema alisema hana taarifa za Serikali kushtakiwa katika Mahakama ya Kimataifa ya The Hague, “Kwa nini wameamua kutushtaki katika Mahakama ya The Hague? Kwani hapa nchini hakuna mahakama au wameona ni bora wavuke mipaka... Kwa sasa siwezi kulizungumzia zaidi suala hilo.”

Wakili wa Kujitegemea, Gaudioz Ishengoma alipotakiwa kuzungumzia hilo alisema anaunga mkono uamuzi wa kituo hicho kuipeleka Serikali kwenye Mahakama ya Kimataifa.

Alisema hilo ndilo eneo sahihi ambalo Serikali inatakiwa kupelekwa kwa sababu ya ukiukaji wa haki za binadamu na kwamba huko ndiko ambako haki inaweza kupatikana.

Hata hivyo, Wakili mwingine wa Kujitegemea, Majura Magafu alipinga hatua hiyo akisema kituo hicho kimekosea kuipeleka Serikali The Hague kwa kuwa imekuwa ikichukua hatua za kisheria dhidi ya makosa mbalimbali ya mauaji ambayo yamekuwa yakitokea, “Kwa mawazo yangu, hawa LHRC wamekosea nadhani wamefanya hivyo kwa masilahi yao binafsi hasa ili kuonyesha kwamba wanafanya kazi,” alisema.

Alisema hata kama Serikali itakuwa imeshindwa kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wauaji, kituo hicho kilitakiwa kuishtaki Serikali katika mahakama za hapa nchini, “Hawa sijui wanataka kutupeleka wapi kwa sababu wananchi wengi wa Afrika wakiwemo wa Kenya wamekuwa wakitaka mashtaka yasipelekwe nje ya nchi, hivi kila kitu tunawategemea Wazungu kwa sababu gani hasa?”