Thursday, February 6, 2014

UNAAMBIWA ZITTO KABWE AIBUKA NA DVD MATATA SANA, SOMA UJUE INAHUSU NN,




Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.
WAKATI Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, akijipanga kuanza ziara katika mikoa kadhaa nchini kujibu mapigo ya tuhuma dhidi yake zilizotolewa na baadhi ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwenye ziara ya
Operesheni M4C Pamoja Daima, mbunge huyo ameibuka na DVD inayowananga viongozi wa CHADEMA.
Vyanzo vyetu vya habari vilisema kuwa DVD hizo zitasambazwa kwenye mikoa na maeneo yote atakayofanya mikutano ya hadhara mbunge huyo, kama moja ya harakati na mikakati ya kujisafisha na tuhuma za usaliti zinazomkabili ndani ya chama.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa DVD hizo zinatengenezwa kwenye kampuni moja iliyopo eneo la Kariakoo ambayo imepewa tenda ya kuchapa nakala 10,000 na kampuni nyingine zaidi ya tatu, nazo zimepewa tenda ya kuchapa DVD hizo kwa idadi tofauti.
Hata hivyo jambo la kushangaza ni kwamba katika jaradio la DVD hizo kuna rangi ya njano, nyeupe, bluu nyepesi, bluu nzito pamoja na bendera ya taifa.
Rangi zilizotumika kwenye jaradio hilo hazina uhusiano na rangi za bendera ya CHADEMA wala chama chochote cha siasa nchini.
Mbali ya jaradio hilo kupambwa na rangi hizo, pia limepambwa na picha kadhaa za mikutano aliyopata kuifanya mwanasiasa huyo katika maeneo mbalimbali na nyakati tofauti nchini, huku picha kubwa ikimwonyesha Zitto akiwa amevalia suti huku akitabasamu.
Jaradio hilo pia limezungukwa na maandishi mbalimbali ambayo yanasomeka:
‘Uadilifu, Uzalendo na Uwajibikaji, ndio silaha yetu katika kutetea wanyonge na maskini wote wa Tanzania, tuungane kwa pamoja.’  ‘Tanzania Kwanza’

Maandishi mengine makubwa yanamtambulisha mbunge huyo ambayo  nayo yanasomeka:
‘Zitto Zuberi Kabwe, Mtetezi wa Wanyonge, Tumaini la Maskini wa Tanzania”
Jaradio hilo pia limeweka mawasiliano ya mbunge huyo ya simu ya mkononi, barua pepe, Facebook na Twitter.

Hakuna maelezo yanayoonyesha kama DVD hizo zinauzwa au zinatolewa bure.
Ndani ya DVD
DVD hizo ambazo nakala tunayo, zinaonyesha picha ya mikutano ya hadhara ya mbunge huyo aliyoifanya mkoani Kigoma mara baada ya Kamati Kuu (CC) ya CHADEMA kumvua nyadhifa zake na Mahakama Kuu kushikilia hatima ya uanachama wake baada ya kukabiliwa na tishio la kuvuliwa uanachama.

Kwa mujibu wa DVD hizo, katika moja ya mikutano ya mkoani Kigoma, Zitto anasikika akiuambia umati wa wafuasi wake waliofurika kumsikiliza akieleza chanzo cha mgogoro wake na CHADEMA ni msimamo wake wa kuhoji hesabu za fedha za vyama vya siasa, kikiwemo CHADEMA na kumuagiza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kufanya uhakiki.

Kama ambavyo amepata kukaririwa mara kwa mara, Zitto ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) anasema CHADEMA ilimtaka awajulishe kwanza kabla ya kumuagiza CAG kufanya ukaguzi ili kutoa fursa ya kuweka hesabu zao vizuri.

DVD hiyo pia inamuonyesha Zitto akisema sababu nyingine ya ugomvi wake na CHADEMA ni dhamira yake ya kutaka kuwania uenyekiti wa CHADEMA, nafasi ambayo kwa sasa inashikiliwa na Freeman Mbowe, Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.

Huku akishangiliwa na maelfu ya wafuasi wake, baadhi wakiwa na mabango ya kumsifia, Zitto anasema hajawahi kupewa fedha na CCM kuisaliti CHADEMA na kuongeza kwamba atakuwa wa mwisho kutoka ndani ya chama hicho alichojiunga nacho akiwa na umri wa miaka 16.

Dk. Kitila Mkumbo naye yumo

DVD hiyo pia inamuonyesha aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu na Baraza Kuu la CHADEMA, Dk. Kitila Mkumbo, akieleza sababu za yeye kutaka kujiuzulu kabla ya Kamati Kuu kuamua kumvua uanachama.

Dk. Kitila pia anaonekana  kwenye DVD hiyo akielezea waraka ulioandikwa na Samson Mwigamba ambao ulinaswa ukielezea mikakati ya kutaka kuung’oa uongozi wa Mbowe kwenye nafasi ya uenyekiti.

Kwa kifupi maelezo ya Dk. Kitila ni  yale aliyopata kuyatoa siku yeye na Zitto walipofanya mkutano na vyombo vya habari katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam wakitetea waraka huo kwamba haukuwa wa uasi kama ilivyotafsiriwa na CHADEMA.

Wiki iliyopita gazeti hili liliibua mkakati  unaodaiwa kufadhiliwa na  Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa kutaka kumtumia Zitto kupambana na CHADEMA waziwazi.

Katika mkakati huo CCM inadaiwa kutaka kukodisha helikopta ya kumpeleka Zitto katika mikoa minne kwa gharama ya sh milioni 50, mara tu baada ya CHADEMA kuhitimisha Operesheni yao ya M4C Pamoja Daima.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka vyanzo vilivyo karibu na Zitto na CCM, yeye na chama hicho sasa wana adui mmoja – CHADEMA; na wameamua kujibu mapigo baada ya kuridhika kwamba kwa vyovyote Zitto amekwisha kupoteza uanachama wake katika CHADEMA.

Nia yao ni kumtumia Zitto kuleta mpasuko katika CHADEMA, na kufunika mjadala wa mgogoro wa CCM, kero za wananchi na mchakato wa Katiba mpya.

Zitto ambaye alivuliwa nyadhifa zake zote ndani ya CHADEMA – Naibu Katibu Mkuu Bara, Mjumbe wa Kamati Kuu, Mjumbe wa Baraza Kuu na Naibu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni – anatarajia kutumia helikopta yenye uwezo wa kubeba watu wanne, ambayo inadaiwa kukodishwa na wapinzani wa CHADEMA.

Kwa mujibu wa habari hizo, lengo la ziara ya Zitto ni kujibu mapigo ya CHADEMA, hasa katika maeneo ambayo baadhi ya makada na viongozi wa chama hicho wamepita na kuzungumzia hatima yake kisiasa, hasa walipojibu maswali ya wananchi kuhusu sakata lake kuvuliwa uongozi kwa tuhuma za usaliti, na hatimaye Zitto kwenda mahakamani kuzuia chama kujadili uanachama wake.

Katika kesi ya msingi, Zitto aliyewahi kuwa maarufu akiwa kiongozi wa CHADEMA, anaomba arudishiwe nyadhifa zake zote, na apatiwe nakala za uamuzi wa Kamati Kuu (CC) ili aweze kukata rufaa Baraza Kuu.

CHANZO NI TANZANIA DAIMA

No comments:

Post a Comment