Monday, January 6, 2014

JACK PATRICK ALIYEKAMATWA NA MADAWA YA KULEVYA MAPYA YAIBUKA, LUGHA NAYO GONGANO, KESI KUSIKILIZWA 2016:

Jacqueline Patrick ‘Jack’. Mrembo huyo alikamatwa Desemba 19, mwaka jana katika Uwanja wa Ndege wa Macau akitokea Bangkok, Thailand akiwa na kete 57 (kilo 1.1) za unga aina ya heroin tumboni zikiwa na thamani ya shilingi milioni 300. 
TAARIFA MBICHI
Taarifa mbichi kabisa zinadai kwamba, Jack amepewa mwaka mmoja na nusu (siku 447) ajifunze lugha inayozungumzwa na watu wa Macau (Kireno) ambayo ndiyo itakayotumika mahakamani wakati kesi yake itakapoanza kuunguruma.


Dawa za kulevya alizokutwa nazo Jack Patrick.
Sheria ya kisiwa hicho inasema kuwa mshitakiwa yeyote atakayefikishwa kortini, kesi yake haitasikilizwa mpaka majaji wakubali kwamba anajua lugha hiyo na si kinyume na hapo.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, mwalimu maalum anayejua Lugha za Kiingereza na Kireno ndiye atakayemfundisha Jack mpaka atakapojua.

AKIJUA MAPEMA ITAMSAIDIA
Habari za ndani kutoka vyanzo vya uhakika nchini humo zinasema kwamba, kama Jack angekuwa anakijua Kireno angepandishwa kizimbani mara baada ya upelelezi kukamilika, Machi mwaka huu.

KIFUNGO CHA CHINI MIAKA 16
Habari nyingine mpya kutoka Macau zinasema kuwa, sheria za eneo hilo kuhusu makosa ya kukutwa na madawa ya kulevya, mtuhumiwa akitiwa hatiani kifungo cha chini ni miaka 16 kulingana na mwenendo wa kesi.

SERIKALI YA TANZANIA YASUBIRI ORODHA…
Juzi, Uwazi liliwasiliana kwa simu ya mkononi na Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, Godfrey Nzowa na kumuuliza kuhusu nini kinaendelea kati ya serikali na utawala wa Macau kufuatia Mtanzania, Jack Patrick kunaswa na unga nchini humo.

Nzowa: “Aaah! Sisi tumetuma maswali yetu kule (Macau) kupitia Polisi wa Kimataifa (Interpol), tumetaka kujua kama huyo binti (Jack) amewataja vigogo waliomtuma ni majina gani wanayo.
“Ndiyo tunasubiri majibu yao ili tujue nini kinaendelea kule. Kama aliwataja watu tutaanza kuwafuatilia mara moja maana lazima kuna vigogo nyuma yake.”

KWA NINI MABOSI WA KUBEBA UNGA HUWA HAWATAJWI?
Kinachomshangaza Kamanda Nzowa ni usiri wa watu wanaodaiwa kukamatwa na unga kufunga vinywa vyao kuwataja vigogo waliowatuma.
Inadaiwa moja ya kiapo kikubwa kabla mtu hajaanza kuwa ‘punda’ (kubebeshwa madawa ya kulevya) ni kusema ‘piga, ua, galagaza’ katu hawezi kutaja wahusika wenye mzigo.

“Unajua kwa sababu gani? Wale wanaobeba wanaambiwa mkikamatwa msitutaje hata iweje ili tufanye mipango ya kuwatoa. Sasa mtu anaona nikitaja sintatoka, ndiyo anaamua kuendelea kuishi na siri yake halafu na wao wakubwa wao wanakuwa hawana habari nao,” alisema Nzowa.

KUMBE JACK ALIPEWA MAJI YA MOTO
Habari zaidi zinasema kuwa, siku ya tukio la kukamatwa, Jack alikataa kwamba hajabeba kete za unga tumboni, askari wa uwanjani wakampa maji ya moto ili anywe.
“Kwa mtu aliye na kete tumboni, hawezi kukubali kunywa maji ya moto kwani huyeyusha kete zilizomo ndani na kuweza kusababisha kifo chake.

“Jack alikataa kunywa maji ya moto, hilo likachangia askari kuamini ana kete tumboni, ndiyo maana walimpeleka chooni kuzitoa kitaalam,” kilisema chanzo.
RAY C AWASHANGAZA WENGI
Kufuatia sakata la Jack, hivi karibuni, staa wa muziki wa kizazi kipya Tanzania, Rehema Chalamila ‘Ray C’ aliingiza kwenye mtandao wake wa kijamii akitoa maoni kwamba Jack apewe adhabu kali zaidi ya kifungo (pengine kunyongwa) hali iliyowashangaza wengi waliotembelea mtandao huo.

Baadhi ya watu waliozungumza na Uwazi baada ya staa huyo kuingiza mawazo yake walimshutumu wakisema alitakiwa kutafakari upya.
“Yule dada (Ray C) hakutakiwa kumtakia mwenzake mabaya zaidi, kama yeye aliathirika na madawa na amepona anatakiwa kuwa balozi kwa wengine na si kuwahukumu wenzake,” alisema Joan Mushi, mkazi wa Sinza ‘E’ jijini Dar.
WAZIRI MEMBE VIPI?
Juzi, Uwazi lilimtafuta Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Kamillius Membe ili azungumze lolote kuhusu sakata la Jack Patrick lakini hakupatikana badala  yake naibu wake, Mahadhi Maalim alisema taarifa za Jack kukamatwa amezisikia  kupitia vyombo vya habari na hana habari kiundani ila bosi wake anaweza kuwa na maelezo zaidi.

WOLPER, AUNT EZEKIEL, WEMA, WANAWINDWA KUWA ‘MAPUNDA’
Wakati Jack akiwa katika mazito hayo, habari ambazo zilifika kwenye dawati la Uwazi dakika za mwisho zinasema mastaa wa filamu za Bongo, Jacqueline Massawe Wolper, Aunt Ezekiel Grayson na Wema Isaac Sepetu wamekuwa wakitolewa udenda na vigogo wa unga. 

Vigogo hao wamekuwa wakihaha kutafuta namna ya kuwaingiza mastaa hao kwenye ‘chaneli’ yao ili wawe mapunda wa kubeba kete za unga kupeleka ughaibuni wakiamini kuwa, mastaa hawakamatwi hovyo uwanja wa ndege, hususan wa Dar es Salaam.
-GPL

No comments:

Post a Comment