Saturday, November 9, 2013

USHAHIDI WA PICHA,KASEJA AFUNGA NDOA NA YANGA KWA MIAKA 2 KWA DAU LA MILIONI 40


Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam KIPA hodari nchini, Juma Kaseja leo amesaini Mkataba wa miaka miwili na klabu ya Yanga SC kwa dau la Sh, Milioni 40. Kaseja amesainshwa na vigogo wa Usajili wa Yanga, Abdallah Ahmed Bin Kleb na Seif Ahmed ‘Magari’ mbele ya Meneja wake, Abdulfatah Salim Saleh Ilala mjini Dar es Salaam. Kaseja sasa anakwenda kuungana na makipa wawili aliowahi kufanya nao kazi Simba SC, Ally Mustafa ‘Barthez’ na Deo Munishi ‘Dida’.
Juma Kaseja akisaini Yanga huku akishuhudiwa na Seif Magari. Nyuma ni Meneja wake, Abdulfatah Salim Saleh
Hii inakuwa mara ya pili Kaseja kusajiliwa Yanga, baada ya awali kusajiliwa mwaka 2009 akitokea Simba SC ambako baada ya msimu mmoja wa Mkataba wake kumalizika akaachwa na kurejea Msimbazi. Kaseja aliachwa Simba SC mwishoni mwa msimu kwa madai kiwango chake kimeshuka na amelazimika kuukosa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Bara, ingawa sasa baada ya kumwaga wino Yanga anarudi kazini Januari. Kikubwa kilichoisukuma Yanga SC kumsajili kipa huyo ni uzoefu wake katika michezo ya kimataifa na inataka inufaike naye katika Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani.
Kaseja na Bin Kleb, nyuma Abdulfatah 

Kaseja aliibukia sekondari ya Makongo, Dar es Salaam ambako aliitwa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys mwaka 2001 chini ya kocha Mnigeria, Ernest Mokake aliyekuwa akisaidiwa na mzalendo, Juma Matokeyo, wote sasa marehemu. Mwaka huo huo alisajiliwa na Moro United aliyoichezea hadi mwaka 2003 alipohamia Simba alipopiga kazi hadi 2009 akaenda Yanga na kurejea mwaka mmoja baadaye ambako alifanya kazi hadi mwishoni mwa msimu uliopita alipotupiwa virago.

No comments:

Post a Comment