Thursday, March 28, 2013

MBUNGE JIMBO LA CHAMBANI AFARIKI DUNIA GHAFLA MARA BAADA YA KUANGUKA KWENYE KIKAO CHA KAMATI YA BUNGE

  • Kutokana na msiba huu, Spika wa Bunge Mhe. Anne Makinda ametoa taarifa akifahamisha kuwa shughuli zote za Kamati za Bunge zimearishwa hadi jumanne tarehe 2 Aprili, 2013. Marehemu ataangwa kesho tarehe 29 Machi, 2013 saa 2:30 asubuhi katika ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam na kusafirishwa kwa ndege kwenda Pemba saa nne asubuhi ambapo mazishi yatafanyika mchana nyumbani kwake Chambani, Pemba. 
  • Taarifa ya Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julis Mtatiro inasema kuwa Msafara utaondoka Karimjee saa 4:00 kuelekea uwaja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) ambapo msafara wa ndege mbili utaondoka kwenda Pemba. Saa 7 mchana mazishi yatafanyika huko Pemba yakiongozwa na viongozi wa Serikali na Wabunge.

Picture
Salim Hemed Khamis
Mbunge wa Chama Cha Wananchi (CUF) Jimbo la Chambani, Salim Hemed Khamis amefariki dunia.

Jana taarifa za habari zilitangazwa kwamba Mbunge huyo alianguka jana ghafla akiwa katika kikao cha kamati ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa katika ofisi ndogo za bunge jijini Dar es salaam wakati kamati hiyo ikiendelea na kikao chake.

Mbunge huyo ambaye siku za hivi karibuni ametoka nje ya nchi kwa matibabu ya afya yake amefikwa hali hiyo na kubebwa na baadhi ya wabunge kwa kushirikiana na baadhi ya wandishi wa habari kutolewa nje ya chumba cha mkutano na kupelekwa hospital ya taifa ya Mhimbili kwa uchunguzi na matibabu zaidi.

Mwenyekiti wa kamati ya bunge ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa Edward Lowasa jana amethibitisha kutokea kwa tukio hilo la kuanguka ghalfa.

Mbunge huyo jana alikutwa na masahibu hayo jana na alikimbizwa hospitalini kwa matibabu ambako alilazwa katika 

chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi wa karibu (ICU).

Wajumbe wa kamati hiyo wakiongozwa na Mwenyekiti wake, Edward Lowassa, na Makamu Mwenyekiti, Mussa Hassan Zungu na baadhi ya wajumbe walimtoa nje ya ukumbi na kumpepea kwa kutumia magazeti na majarida.

Hata hivyo, hali yake ilizidi kuwa mbaya huku akizungumza kwa tabu kuwa alikunywa dawa za shinikizo la damu (BP) kabla hajala chochote na hivyo kuzidiwa.

Wabunge hao na maofisa wa Bunge, waliendelea kumpepea ili apate ahueni, lakini hali ilizidi kuwa mbaya na kushindwa kuongea kila alipoulizwa jambo.

Walimbeba na baada ya muda waliomba msaada kwa wanahabari waliokuwapo eneo hilo huku wakiwazuia wasipige picha za tukio hilo kwa maelezo kuwa si kila kitu ni habari.

Waandishi watano walisaidiana na wabunge hao kumbeba kwa kupitia mlango wa dharura na alipakizwa kwenye gari la ofisi ya Bunge lenye namba za usajili STK 2178 likiongozwa na pikipiki ya polisi yenye namba za usajili PT 2591.

Gari iliyombeba Mbunge huyo iliondoka kwenye ofisi hizo saa 5:15 asubuhi na habari zilizopatikana baadaye zilieleza kuwa alipelekwa Muhimbili kwa matibabu zaidi.

Baadhi ya wabunge walisema kuwa Khamis akiwa amekaa, ghafla alianza kutapika huku akilalamika kuwa hajisikii vizuri baada ya kunywa dawa za BP na hali yake kubadilika na walisaidiana kumtoa nje ya chumba cha mkutano.

Pamoja na wabunge hao pia, alikuwapo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi.

Waliomsindikiza hospitalini ni Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Amour Arfi (Chadema) na Mbunge wa Gando, Khalifa Suleiman Khalifa (CUF).

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kurejea kutoka Muhimbili, Khalifa alisema Khamis alipokewa na alikuwa anaendelea kupatiwa matibabu.

Khalifa alifafanua kuwa Khamis anasumbuliwa na tatizo la shinikizo la damu.

Kwa mujibu wa gazeti la Nipashe la leo limeandika kuwa, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Edward Lowassa, alisema hali yake ilikuwa inaendelea vizuri na kuthibitisha kuwa amelazwa ICU. Lowassa alisema kuwa miezi mitatu iliyopita Khamis alikuwa India kwa matibabu. Ofisa Uhusiano wa Muhimbili, Aminiel Eligaesha, alipoulizwa kwa njia ya simu, alithibitisha kuwa mbunge huyo kupokewa hospitalini hapo na kuongeza kuwa alipatiwa matibabu na anaendelea vizuri. Hata hivyo, alisema taarifa kamili itatolewa na ofisi za Bunge.

Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, alisema hadi jana jioni mbunge huyo alikuwa bado ICU chini ya uangalizi wa madaktari. “Bado yuko ICU. Wanamwangalia. Presure (shinikizo la damu) iko juu, tunampumzisha kidogo,” alisema Joel akijibu swali la NIPASHE kuhusu maendeleo ya afya ya mbunge huyo. Akijibu swali iwapo kuna mpango wowote wa kumpeleka mbunge huyo kupatiwa matibabu zaidi nje ya nchi, alisema: “Tunasubiri ushauri wa madaktari.”

--
Chanzo cha taarifa hii: Salma Said, Zanzibar.

No comments:

Post a Comment