Wednesday, September 19, 2012

TAMKO LA UBALOZI WA MAREKANI NCHINI TANZANIA KUHUSU FILAMU YA INNOCENCE OF MUSLIM

Tunapongeza matamko yaliyotolewa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa dini ya Kiislamu nchini Tanzania wakilaani kushambuliwa kwa wanadiplomasia wa Kimarekani huko Libya na vitendo vingine vilivyo kinyume na imani za kidini, huku wakihimiza kuwepo kwa utulivu na majadliano ya amani.

Ikiwa nchi ya watu wa imani zote, wakiwemo mamilioni ya Waislamu, Marekani inaamini kwa dhati kabisa katika uhuru wa watu kuabudu na kufuata imani zao za kidini. Kama alivyosema Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Bibi. Hillary Rodham Clinton siku ya Ijumaa, Septemba 14, 2012, Serikali ya Marekani haihusiki kwa vyovyote vile na filamu ya udhalilishaji inayosambazwa katika mtandao wa internet ambayo ndiyo imesababisha maandamano katika nchi mbalimbali. Tunapinga na kulaani maudhui yake yasiyo na chembe ya heshima na ujumbe wake wa kuudhi na kuleta chuki.

Marekani na Tanzania ni nchi zenye hazina kubwa ya kuheshimu uhuru wa dini na watu wake wa dini mbalimbali kuvumiliana. Ubalozi wetu jijini Dar es Salaam una fahari kubwa kushirikiana na viongozi wa dini zote. Programu za kujenga maelewano, na mabadilishano ya kitamaduni na kielimu na Watanzania wa imani zote, ikiwemo Waislamu, ni jambo linalopewa kipaumbele cha juu na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania.

Programu zetu za kusaidia maendeleo zinatuwezesha kufanyakazi na viongozi wa kidini, mashirika ya kiraia na sekta binafsi na kusaidia jitihada zao za kujenga mustakabala Mwema kwa Watanzania wote.

Kwa mfano, kwa kupitia Millennium Challenge Corporation (MCC), serikali ya Marekani inafadhili mradi wa kupeleka Zanzibar umeme wa megawati 100 kupitia nyaya zinazolazwa baharini ili kuboresha upatikanaji wa umeme visiwani humo. Kwa kupitia Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) mradi wa kutokomeza Malaria visiwani Zanzibar umepunguza kwa kiwango kikubwa matukio ya ugonjwa huo Zanzibar.

Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na UKIMWI (PEPFAR) umekuwa ukiendesha programu mbalimbali za kukabiliana na VVU/UKIMWI zinazookoa Maisha ya maelfu ya watu nchini Tanzania. Hali kadhalika, Mpango wa kusaidia kilimo na usalama wa chakula unaoendeshwa na USAID (Feed the Future) unafadhili shughuli mbalimbali za kilimo na kiuchumi zinazolenga kuinua ubora wa Maisha wa Watanzania wote - ambao miongoni mwao Waislamu ni sehemu kubwa.

Katika kujenga na kuimarisha mahusiano baina ya watu wa nchi hizi mbili, Ubalozi wa Marekani umekuwa ukiwakaribisha vijana wa Kiislamu katika maktaba yake kuu na katika maktaba ndogo (American Corners) zilizopo Unguja, Pemba na Mwanza.

Aidha, Ubalozi umekuwa ukiendesha programu mbalimbali za kuwafikia Watanzania huko waliko (outreach programs) na kuwa na majadiliano nao yaliyo wazi. Mfuko wa Balozi wa Marekani wa Kuhifadhi Amali za Kitamaduni (The Ambassador's Fund for Cultural Preservation) umekuwa ukitupa fursa ya kuonyesha jinsi Marekani inavyoheshimu na kuthamini hazina ya kipekee ya kitamaduni na kihistoria ya Tanzania.

Toka mwaka 2002, Watu wa Marekani wametoa jumla ya Dola za Kimarekani 1,090,000 katika kusaidia hazina za kiutamaduni na kihistoria za Tanzania, ikiwa ni pamoja na Miskiti ya Kizimkazi na Micheweni huko Zanzibar na magofu ya Kilwa Kisiwani. Hali kadhalika, Watu wa Marekani wametoa zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 49 kuchangia mradi wa matumizi ya teknolojia ya kisasa ya habari katika kufundishia mashuleni (Tanzania 21st Century Education Program -TZ21) unaotekelezwa huko Zanzibar na Mtwara kupitia USAID.

Kukuza majadiliano ya wazi na ukweli pamoja na kujenga maelewano ndiyo dhamira yetu kuu. Tumedhamiria kwa dhati kufanyakazi na Watanzania katika kuendeleza malengo hayo.

----
Tamko limenukuliwa kutoka, SwahiliVilla blog