Sunday, February 10, 2013

NENO LA LEO KUTOKA KWA MJENGWA


Ndugu zangu,

Leo asubuhi nikiwa kwenye jogging hapa Iringa nilikutana na picha ya watu wazima wawili; wote wameshika baiskeli. Hawaendeshi, wanazikokota.

Mmoja anapandisha, mwingine anashuka. Jua la asubuhi lilikuwa likichomoza. Anayeshuka anapigwa na jua usoni, anayepanda, mgongoni.

Niliipiga picha ile. Kisha nikaendelea kufanya jogging huku nikitafakari kuhusu maisha. Kuwa katika dunia hii, kama ilivyokuwa kwa watu wale wawili; kuna kupanda na kushuka.

Kuna masikini na matajiri. Masikini anaweza kuwa tajiri na tajiri anaweza kurudi kwenye umasikini. Hakuna aliyezaliwa kuwa masikini daima na kinyume chake. Ni mazingira tu. Kama mwanadamu, ukisema mimi siwezi hutaweza, na kinyume chake.

Na wengi walioshinda katika maisha humu duniani wana historia ya kushindwa pia. Wengine wamepata kushindwa mara nyingi, lakini, hawakukata tamaa. Walianguka, wakasimama kuendelea kupambana.

Ndio, katika dunia hii, mwanadamu unatakiwa upambane mpaka pumzi yako ya mwisho. Kwenye Uchina ya kale kulikuwa na mwanafalsafa kwa jina la Comfucius. Katika mafundisho yake mengi aliyopata kumpa mwanafunzi wake Tzu Kung, mojawapo linahusu dhana ya utajiri na mahusiano yake na umasikini.

Comfucius anasema; ukimwona mtu tajiri(aliyefanikiwa kimaisha),basi tamani kuwa kama yeye, lakini, ukimwona aliye masikini, basi, jitafakari wewe mwenyewe.

Kwa mwanafalsafa Comfucius, dhana ya utajiri haikuwa na maana kuwa na mali pekee, bali, pamoja nazo, ni uwezo wa mtu kuishi maisha adilifu na yenye fadhila (virtues). Na katika fadhila zote, ile ya unyenyekevu na ukweli ndio chanzo cha fadhila nyingine zote.

Umasikini vilevile, yumkini unaweza kuwa na maana ya kukosa mali na uadilifu. Ndio, mwanadamu waweza kuwa na mali lakini ukakosa uadilifu. Ni dhahiri, katika hali hiyo, hata mwenye mali naye ni masikini sana.

Na hilo ni Neno La Leo.

No comments:

Post a Comment