Saturday, September 8, 2012

BABA WA DKT ULIMBOKA AZUNGUMZIA KUTEKWA KWA MWANANE

Florence Majani, MWANANCHI, Dar es Salaam --  BAADA ya kimya cha muda mrefu, baba mzazi wa kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dkt. Stephen Ulimboka, amekubali kuzungumzia sakata la mwanaye kutekwa, kuteswa, kutibiwa na hatimaye kurejea nchini akisema kwamba kupona kwake ni neema za Mungu, huku akiishutumu Serikali kuwa imewatelekeza Watanzania.

Hii ni mara ya kwanza kwa baba huyo, Stephen Mwaitenda kuzungumza tangu mwanaye alipotekwa, kuteswa na baadaye kutupwa katika Msitu wa Pande, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

“Naishangaa Serikali hii ambayo wananchi wanapigwa na kuuawa bila makosa. Nakumbuka kiongozi aliyeipenda Tanzania ni mmoja na ameshatangulia mbele za haki,” alisema akimaanisha Baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere.

Mwaitenda alitoa kauli hiyo jana baada gazeti la MWANANCHI kumtafuta ili azungumzie habari zilizoenea nchini kwamba mwanaye, amepata kazi nje ya nchi ambapo Mwaitenda alikanusha madai hayo akisema kuwa mtoto wake hawezi kwenda nje ya nchi bila yeye kufahamu... “Pengine ana mipango hiyo, lakini mimi sijui wala sijasikia, lakini atakwenda nje ya nchi kufanya nini? Hizi habari hizo ndiyo nazisikia kwako kwa mara ya kwanza eti Ulimboka anataka kwenda nje ya nchi? Akafanye nini alichokosa hapa Tanzania!”

Wakati mwandishi akiingia nyumbani kwa Mwaitenda, Ubungo Kibangu, Dar es Salaam, alipishana na Dkt. Ulimboka akiwa kwenye gari na wenzake, wanne. Hata hivyo, hakufanikiwa kuzungumza naye.

Kuhusu tukio la kutekwa, kuteswa na kutupwa katika Msitu wa Pande, Mwaitenda alisema: “Mpaka sasa, tumeiona kazi ya Mungu, ile ni neema ya Mungu kwa sababu wewe uliona wapi mtu akapigwa namna ile halafu akapona kama si kwa neema tu.”

Alisema alimkanya mtoto wake huyo aachane na masuala ya migomo na siku chache baada ya onyo lake ndipo akatekwa na kujeruhiwa vibaya, “Nilimkanya kabisa kuhusu mambo ya migomo hasa baada ya kuniambia kuwa amechaguliwa kuwa Msemaji Mkuu wa Madaktari wenzake na kwa bahati mbaya ndiyo yakatokea hayo yaliyotokea,” alisema.

Alielezea kushangazwa kwake na watu waliompiga mtoto wake akisema, hajui walikuwa wanataka nini. Alisema hakuwa na uhasama na mtu yeyote kuanzia kazini kwake hata kwa marafiki zake, “Mpaka sasa nashindwa kuelewa kwa nini waliamua kumpiga, kwa sababu kwa ninavyomjua Steven, hajawahi kuwa na ugomvi na mtu tangu anasoma shule ya msingi mpaka anamaliza chuo kikuu. Sijawahi kupata mashtaka kuwa amegombana na mtu. Nashangaa haya yanayotokea leo.”

Akitoa wasifu wa mwanaye huyo alisema tangu utoto wake, Daktari huyo alikuwa mtulivu na mwenye upeo wa hali ya juu. Alisema anasikitishwa mno na yaliyompata akisema kwamba siku moja ukweli utawekwa wazi  kwani siku zote kazi za Mungu na kazi za shetani haziwezi kuchangamana, “Kama mafuta na maji, ukiyachanganya... mafuta yatakuwa juu na maji yatabaki chini. Najua siku moja Mungu ataweka wazi ukweli,” alisema.

Kuhusu afya ya Dkt. Ulimboka, Mwaitenda alisema ingawa yeye si daktari, lakini anamwona mtoto wake kuwa yu mwenye afya na kuongeza kuwa hata mwanaye huyo amekuwa akisema kwamba sasa ana afya njema.

Hali nyumbani kwa Mwaitenda

Baada ya kufika nyumbani kwa mzazi huyo wa Dkt. Ulimboka, mwandishi alikaribishwa vyema na mzazi huyo ingawa alimtahadharisha kwamba endapo angekutana na Daktari huyo hapo au ndugu zake, wangemfukuza, “Una bahati ungewakuta hapa watoto wangu tusingezungumza. Hata hawa mabinti zangu wakikukuta, hatutaendelea na mazungumzo....”

Hivyo ndivyo ilivyotokea kwani baada ya kuelezea hayo, mabinti wake wawili walitokea na mmoja akaanza kwa kusema... “Shikamoo Baba, umesharudi? Huyu nani?”

Mzee Mwaitenda, kwa bashasha aliwatambulisha mabinti hao... “Huyu ni Florence... mwandishi wa MWANANCHI...” Hata kabla hajaendelea binti huyo na mwenzake walimshika mkono na kumwamuru atoke nyumbani hapo mara moja.

“Haya dada toka, toka, mmeshindwa kuandika kuhusu mwandishi mwenzenu aliyekufa (Daudi Mwangosi), mnakuja kutufuata mpaka huku Kibangu.... mtazame miguu ilivyomchafuka kwa vumbi kwa kushadadia ya watu, toka kabla sijakupiga makofi,” alisema mmoja wa mabinti hao.

Kauli ya Dkt. Mkopi, Prof. Kahamba


Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dkt. Namala Mkopi ambaye alikuwa karibu na Dkt. Ulimboka wakati wa mgomo wa madaktari nchini, alisema tangu waonane aliporejea nchini kutoka Afrika Kusini, hajawasiliana tena.

“Hatujawasiliana naye,” alisema Dkt. Mkopi na kusema kulingana na ukubwa wa tatizo lililompata, hakuwa na mpango wa kumsumbua, bali kumwacha apumzike hadi atakapokuwa amejisikia mwenyewe kurejea kazini.

Aliyekuwa kiongozi wa jopo la madaktari waliomhudumia, Profesa Joseph Kahamba alisema, hajawahi kuonana wala kuwasiliana na Dkt. Ulimboka tangu alipopelekwa Afrika Kusini, Juni mwaka huu.